Na Mwandishi Wetu
TAASISI ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW) na Mamlaka ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) zimejidhatiti kuimarisha ushirikiano ili kuzalisha walimu wa ufundi stadi nchini.
Mkuu wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima (TEWW)Prof. Philipo Lonati Sanga amesema hayo wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya Miaka 50 ya Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.
Prof Sanga amesema katika kipindi cha Machi mwaka huu, TEWW imepeleka wanafunzi 100 katika Chuo cha Ualimu wa Ufundi Stadi Morogoro(MVTTC) wanaosoma ngazi ya Astashahada na Stashahada ya Ualimu wa Ufundi.
Amesema Hati ya Makubaliano ya ushirikiano kati ya Taasisi hiyo na VETA tarehe 01 Julai, 2024 imewezesha ushirikiano katika kubadilishana wataalamu na miundombinu ya kufundishia na kjifunzia na hatimaye kugusa maisha ya makundi mbalimbali ya watanzania.
Aidha, VETA kwa kushirikiana na TEWW zimehusika katika maandalizi na mafunzo ya walimu wa ufundi na ufundi stadi ili kuhakikisha kwamba sekta ya elimu ya watu wazima na mafunzo ya ufundi inakuwa na walimu waliobobea, wenye uwezo wa kufundisha kwa njia ya kitaalamu na kwa ufanisi pamoja na kuandaa Mitaala ya Mafunzo kwa Walimu wa Ufundi na Ufundi Stadi.
Maeneo mengine ya ushirikiano ni pamoja na kuandaa na kuboresha mitaala ya mafunzo kwa walimu wa ufundi na ufundi stadi kuhakikisha kuwa inakidhi mahitaji halisi ya soko la ajira na maendeleo ya kijamii na kiuchumi pamoja na maandiko ya miradi mbalimbali kwa ajili ya kutafuta ufadhili kitaifa na kimataifa.