Sambamba na nchi zote zitakazokuwa na uchaguzi mwaka huu, hata Mafyatu, nchi ya ndotoni, itakuwa na uchuguzi karibuni.
Kama mjuavyo, Fyatu niliahidi ningeshiriki na kushinda kwa kishindo tena bila kuchakachua au kuchakachuliwa kama uchaguzi ungekuwapo na si uchafuzi na uchakachuaji unaokuja soon. Naona wale wanashangaa.
Hamjui fyatu anaweza kufyatuka wakati wowote? Now, why? Nafyatua kimombo msidhani nina PhD ya kununua. Kama akina msukusi na gwajimmy. Juzi, njemba zangu wa vyombo vya ‘uhasama’ walinitonya kuwa mpango wa kunfiyatua aka kuniengua kwa kuniibia kura.
Hivyo, baada ya kugundua kuwa uchakachuaji, sorry, uchaguzi ujao waweza kuishia kuwa uchafuzi baada ya baadhi ya mafyatu kupanga kunipangua, natangaza rasmi sitagombea. Wale walionichangia njuluku ili kuwakomboa, nawataarifu. Njuluku hizi sasa ni zangu. Nitazitumia vizuri kujiuguza baada ya wajumbe kunifyatua mfukoni.
Pia, nitamnunulia Bi Mkubwa ndinga kali kama ile ya Abidulii aache kutishia kunifyatua akidai kujitoa kumemnyina u-first lady ambapo angeanzisha kampuni yake ya ulaji wa dezo, yaani NGO na kutajirika na kutesa kama hana akili nzuri hivyo kuninyima uhouse.
Nilijitoa ufahamu nikamshauri agombee niwe first lad na kujificha nyuma yake, maana mafyatu hawajazoea first lads isipokuwa first ladies. Kagwaya kupigwa mpina, sorry mpini. Najua mmetastuka na kujiuliza: kwanini nimefyatuka nikaamua kuachana na urahis au tiketi ya kufyatua na kutanua kirahisi.
Msisituke. Sababu zifuatazo zilinifyatua nikafyatuka nikaacha ndoto za urahisi nikichelea kufyatuliwa.
Mosi, nani ashiriki ufyatuaji ambao si chochote bali kiini macho, matusi ya nguoni, na ufyatuaji njuluku za mafyatu waliogoma kufyatuka wakafyatua hadi wanafyatuliwa kila upande?
Fyatu si mwanasesere wa kuchezewa na kuchezeshwa na majambazi kama Joyce Wowowo. Si msanii nishiriki mazingaombwe ambapo Timu yenye Uhuru wa Uchakachuaji (Illegally Notorious and enabling Committee (INeC), ilishapitisha fyatu wake ‘ashinde au kushindishwa’ hata kabla ya uchafuzi wenyewe.
Kama humjui mshindi mpaka sasa, nenda kwa matapeli wa kiroho na wapiga ramli wakuibie. Au mnataka nitabiri? Mshindishwa ajaye atakuwa ni mademoiselle na siyo monsieur kwa Kimasai. Hayo, tuyaache.
Pili, kama mgombea tena Fyatu, nataka Tume siyo Timu Huru iliyo uhuru kupiga mipini wagombea tishio kama mimi na kudhulumu na kudhalilisha demokrasia.
Mie siyo Mpino. Hayo, tunawaachia wale waliokubali tokana na kuogopa au kugoma kufyatuka na kufyatua hadi wanafyatuliwa kila mwaka.
Tatu, natangaza. Hakutakuwa na uchaguzi bali uchafuzi wa demokrasia. Uchaguzi ni kuchagua kilicho bora toka kwenye vingine ili kupata kinachofaa zaidi.
Kwa hujuma nilizogundua, hakutakuwa na uchaguzi bali ushindishaji wa wale ambao ningewashinda tena saa moja asubuhi.
Huwezi kuibua kitu kibaya baada ya kukataa kilicho bora kama fyatu, ukasema kuna uchaguzi.
Uchaguzi, kwa tafsiri yake sahihi, ni ule unaohusisha wapigakura, wa wazi, haki (kama alivyosema Masaji Jajiii mkubwa), na wenye ithibati ambapo kura za kupika kula uheshimika na si wale waliowekwa kutangaza dhuluma, uchakachuaji, viini mato, na vurugu.
Nne, nimepata taarifa kuwa hata majini na maruhani yatapiga kura. Sijui itakuwaje wadudu nao watakapoamua kupiga kura hasa ikizingatiwa kuwa ni viumbe wachafu na wengi.
Kwa vile sina mahusiano na viumbe hawa habithi, sitegemei kupata kura zao ukiachia mbali kuwa hawa mashetani si raia wa kaya yetu ya Fyatuland.
Nasikia wengi ni raia wa kaya ya kufikirika iitwayo Bongolaland ambayo iliangamizwa na huu mchezo mchafu miaka zaidi ya milioni nyingi zilizopita.
Tano, naogopa kushiriki dhambi ya ujambazi, uhujumu, na wizi wa njuluku za mafyatu. Kwa nini kuunguza mabilioni kwenye kiini mato na kituko ambacho matokeo yake yameishajulikana hata kwa kunguru wa India kabla ya uchaguzi, sorry, uchafuzi wenyewe? Mfano, Timu ya Uchafuzi imetangaza kutoa ndinga kwa kila mgombea!
Unawezaje kuwa na uchaguzi bila uwazi na ukweli? Hawa, wanapewa ndinga wakati mteule anapeta kwa njuluku na pipa vyote vya mafyatu akimwaga hongo, sorry, misaada!
Haki iko wapi hapa? Unawezaje bila kuwa na tume huru ila timu huru ya kuzuia uhuru wa wengine?
Unawazaje kuwa na uchaguzi ambapo refa ni mchezaji, mshika kibendera, na kamisaa? Unawezaje kushiriki uchaguzi ambapo mteule anapewa nyundo awatwange washindani wake tena waliofungwa mikono nyuma?
Sita, naogopa kushiriki israfu ya mali za mafyatu mfano, kutoa ndinga kwa ‘wagombea’, wengi si wagombea bali wambea, wasindikizaji, na vikaragosi wa chata twawala, waliowekwa na mteule ili kuwazuga mafyatu na kutufanya wagombea tishio tupigwe mipini wahalalishe haramu yao.
Jiulize. Inakuwaje ninapatikana ndinga za kuwahonga wanasiasa lakini za wagonjwa hazitoshi? Kwanini zisipigwe mnada na kuwanunulia mafyatu matrekta na kuwapa kwa mkopo ili tuongeze uzalishaji badala ya kuongeza udhalilishaji na ulaji?
Kwa vile nina mikakati mipya, sitasema mengi bali kujiandaa kuleta mapinduzi ambayo yatawafyatua mafyatu waache kugoma kufyatuka na kuendelea kufyatuliwa na wale viherehere waliojitoa ufahamu. Hivi nimesemaje?