FYATU MFYATUZI: Walichagua mbung’o wakidhani mbunge!

Mbung’o, chafuo, au ndorobo au tsetse fly kwa kimasai ni mdudu asababishaye ugonjwa hatari wa malale kwa wanadamu na nagana kwa wanyama. Kama inzi wengine, mbung’o si hatari tu bali mchafu na mwenye kueneza maradhi mbali na kuchafua vyakula. Je, wajua mja aweza kuwa mbung’o? Kuna kisa kilitokea kwenye kaya ya Fyatuko.

Katika kisa hiki, mafyatu waliokataa kufyatuka na kuwafyatua wanaowafyatua, walichagua mbung’o wakidhani mbunge kuwawakilisha kumbe waishie kulala na kufyatuliwa kiasi cha kushindwa kufyatuka wakafyatua. Kila kitu kililala. Afya ililazwa kiasi cha kinamama kujifungulia majiani.

Hospitali na zahanati zilikosa vitendea kazi kama vile madawa na ambulansi ilhali ndata wa Fyatuko wakijinoma na mindinga mipya na bei mbaya hata ambayo hawakuihitaji. Maendeleo yalilala. Elimu ililala. Kila kitu na mafyatu walilazwa kulhali.

Kama vile haitoshi, mbung’o waliyemchagua, hakuishia kuwa mbung’o tu katika maendeleo na afya zao, alisifika kwa kulala mjengoni. Alilala kiasi cha kushindwa hata kuuliza swali au kuchangia au kuibua hoja.

Hoja yake kubwa zilikuwa mbili, kuupiga usingizi na kushobokea mshiko aka posho ya makalio bila kuvitolea jasho lolote wala kustahiki.

Kilichoongeza vilio kwa mafyatu wa Fyatuko ni ile hali ya mbung’o sorry mbunge mbung’o wao kuwa kihiyo wa kutupwa ambaye hakuna alilojua zaidi ya kueneza ugonjwa wa malale.

Siku moja, alihojiwa na kuulizwa nini maana ya mswada. Bila aibu na tokana na ugonjwa wa malale, alijibu kuwa mswaada si chochote wala lolote wala hoja ya kuhagaishwa nayo kuijua.

Kwake, si kitu cha maana japo kazi yake aliyochaguliwa kwayo ilipaswa iwe kutunga sharia ambazo huletwa njengoni kama miswada. Hivyo, alishauri mwandishi wa umbea aachane nayo kwa vile haikuwa na maana kwake!

Je, hili halikuhitaji msaada lau lifunzwe maana ya mswada na umuhimu wake kwa kazi yake na mafyatu lililowafyatua wakalipa ulaji?

Mbung’o huishi kwa kuwachafua waja, kuwasababishia magonjwa, na kunyonya damu ya watu na wanyama. Bila uchafu, uwe wa kijamii au kimfumo na damu iwe ya fyatu au hayawani, hakuna mbung’o.

Hivyo, licha ya mbung’o kuwanyonya mafyatu na kuwasambazia magonjwa, alisifika kwa kuwaaibisha mbele ya jamii kutokana na uzwazwa wake.

Ajabu ya maajabu, hata chata kilichompitisha mbung’o kugombea ubunge ilhali alikuwa bingwa wa kula udohoudoho tena mwenye ubuge usio kifani, kiliwashangaza mafyatu ambao walishindwa kujishangaa wenyewe.

Pamoja na mafyatu kushangaa, kadhalika dunia ya wenye akili iliwashangaa ikiwaza ilikuwaje wakachagua mbung’o bila kuchelea madhara yake wakati kulikuwa na mafyatu waofaa kufyatuka.

Hakuna haja ya kuwacheka mafyatu ukajikuta unajicheka mwenyewe bila kujua. Mafyatu wangewezaje kuacha kushangaza wakati walilala baada ya kuambukizwa ugonjwa wa malale hadi wakaliwa wanajiona?

Unapopata ugonjwa wa malale, huwezi kuwaza, kuhoji, kushuku, kukataa, hata kuchukia. Unatenzwa kwa kadri mtesi wako atakavyo, nawe unaona ni sawa.

Ukijitahidi, badala ya kulalamika wazi wazi, unaishia kung’unika wakati unajua tatizo na suluhu yake. Ama kweli, mbung’o na malale ni balaa ambalo hata adui yako huwezi kumtakia!

Pamoja na kisa hiki kuwa cha kufikirika, kuudhi, na kuhuzuisha, kinafikirisha na kufundisha. Je, ni mafyatu wangapi waliochagua mbung’o wakidhani mbunge? Inakuwaje unamchagua fyatu asiyejua hata kile anachokwenda kufanya huko mjengoni wakati anaonyesha wazi kuwa si hajui tu bali hajijui wala kufaa?

Hapa, ukiliwa na kuambukizwa migonjwa, unashangaa wakati umeamua uliwe? Kama si hivyo, kwanini usimfyatue mbung’o kabla ya kukusababishia magonjwa, hasara, hata vifo? Ni wangapi wamekumbana na kadhia hii tokana na kushindwa kufyatuka na kufyatua?

Je, tunao wangapi wafananao na kufanya kama huyu mbong’o kwenye rubaa za kisiasa za kisasa ambazo zimejaa visa, visasi, na mikasa?

Hebu tudurusu zaidi. Linakujia bambataa na mikelele yake na kukusumbua kwa kukuchafulia mazingira kwa njia ya sauti unalipa kura yako usijue kura ni kula?

Juzi, nililisikia moja likisema eti watu watasoma skuli kuanzia la saba hadi la kumi halafu wakimaliza wasome darasa la kwanza hadi la saba!

Jimbung’o hili la kileo lilikuwa limefungulia miziki ya kipedejee lisilojua hata maana ya ujumbe wake huku likimwaga manonihinoo kama chizi lenye kiherehere lililojitoa ufahamu. Ajabu, hata mafyatu walikwenda kulisikiliza badala ya kulizomea hata kulitimua!

Badala ya kuja na sera, jimbung’o hili, lilikuja na ngebe na ngega na kuwapotezea muda mafyatu. Ajabu jingine, eti na timu ya uchafuzi ililipa mshiko likaeneze malale. Wakati mbung’o kama huyu na wengine kama yeye wakipewa njuluku za kueneza malale, mafyatu waliokuwa wengi, walikuwa wakilia kwa umaskini wa kujitakia!

Du! Wakati najiotea na mbung’o naye ananinyemelea aninyonye damu, kunichafua, na kuniambukiza malale!Silali tena nimekustukia mbung’o na wengine kama wewe. Nyambaff kabisa.