Dk Tulia aahidi kujenga barabara za mitaa kiwango cha lami Uyole

Mbeya. Mgombea  ubunge Uyole,  Mkoa wa Mbeya, Dk Tulia Ackson amesema endapo akipata ridhaa ataondoa  vumbi kwa kuja na mkakati  wa ujenzi wa barabara  za mitaa kwa kiwango cha lami ili  kurahisha shughuli za kiuchumi.

Katika hatua nyingine  amesema atahakikisha  anaondoa changamoto ya tatizo la mgawo wa maji kwa hususani kwa wananchi waishio jirani  na Shule ya Sekondari  Iduda ambako kuna mradi wa kisima  kirefu chenye uwezo wa kuhudumia kaya nyingi.

Dk Tulia  amesema hayo Jumatatu Septemba 29,2025 kwenye mkutano wa kampeni  za kuelekea Uchaguzi  Mkuu Oktoba  29, mwaka huu sambamba  na kuomba kura kwa wananchi.

“Serikali  ya CCM imekuja kivingine kwa kazi ya kuleta maendeleo ya  wananchi  wa Iduda, nimepata ombi lenu la ubovu wa barabara za mitaa  na maji nitakuja na suruhisho  endapo mtatupigia kura za kishindo Oktoba  29, mwaka  huu,” amesema.

Amesema  CCM, ikipata ridhaa itabadilisha taswira ya Uyole  ikiwepo  uwezeshaji  wananchi  kiuchumi, sekta ya kilimo, ujenzi  wa miundombinu  ya afya hususani majengo  ya mama na mtoto nchi nzima.


“Hayo yote yanapatikana  Chama cha Mapinduzi (CCM), ambayo yapo kwenye utekeleza  wa ilani ya uchaguzi 2025, 2030  sasa  ili kuyapata  Oktoba  29, mwaka huu  wananchi mkatiki mafiga matatu  kwa Rais Samia Suluhu Hassn, Dk Tulia na Diwani wenu Joseph Emmanuel, “amesema.

Katika  hatua  nyingine amesema  kwenye  sekta  ya elimu kata ya Iduda Serikali  imefanikisha kujenga  miundombinu  ya vyumba vya madarasa, mabweni ya kisasa ,ujenzi  wa kisima cha maji  na kupandisha  kidato cha  tano na sita.

“Awali wanafunzi  wa pembezoni  waliokuwa wakichaguliwa kujiunga  kidato  cha tano  walikuwa wakitembea umbali mrefu kufuata elimu,lakini baada ya  mimi kuwa mbunge Mbeya mjini nilitoa ombi kwa Rais Samia ambaye  alitoa fedha  za ujenzi,” amesema.

Amesema  lengo  la Serikali  ni kuona wananchi wake wanapata huduma stahiki kwa wakati ikiwepo huduma ya maji safi na salama, elimu, afya barabara na nishati  ya umeme.

Dk Tulia  amefafanua  kuwa kufuatia  uwekezaji  wa miundombinu  kwenye  sekta ya elimu hakuna mzazi atakaye  takiwa kuchangia fedha  za madawati  na ujenzi  vyumba vya madarasa kwa wanafunzi  watakao jiunga  kidato cha kwanza mwaka 2026.

“Hakuna mtoto atakaye changia madarasa wala madawati  tayari serikali imetekeleza  kwa vitendo  kila shule nchini ,lengo ni kuwatua mzigo wazazi na walezi sambamba  na kuja na dira ya mpango wa 2025/2050  wa utoaji elimu bora,” amesema.

“Serikali imeondoa michango kwa wanafunzi  watakao chaguliwa kujiunga  kidato cha kwanza 2026, sambamba kusaidia  mahitaji ya sare  hususani mpango  wa bima ya afya kwa wote kwa kaya zisizo jiweza,” amesema.

Wakizungumza  mara baada ya kuhitimisha  mkutano  wa kampeni  wamesema  hatua  ya  Serikali  kuondoa michango kwa elimu ya sekondari  imewatua mzigo mkubwa  wazazi.

“Kimsingi  tunaona mwanga kwa Serikali  ya CCM  kama ilani ya uchaguzi 2025, 2030  itasimamia mwelekeo huo jambo ambalo  litawezesha wazazi  kusimamia kiwango cha taaluma kwa watoto,” amesema  Subiraga Haule.

Amesema  awali wazazi  wengi walikuwa wakikwepa kuwa endeleza watoto elimu ya sekondari  kutokana na michango  holela na kulazimika  kuwapeleka vyuo vya ufundi kupata ujuzi, lakini ametoa angalizo Serikali kusambaza  walaka wa katazo hilo mashuleni.

Diwani Kata ya Iduda, Joseph Emmanuel  amewataka  wananchi  ifikapo  Oktoba 29, mwaka  huu kujitokeza  kwa wingi kupiga kura kuchagua  wagombea  nafasi ya Rais, wabunge na madiwani  ili kuwezesha  kufikiwa na maendeleo.