Dk Tulia aahidi kuondoa adha ya maji Uyole, ataja mradi wa Mto Kiwira kutatua kero

Mbeya. Mgombea ubunge  Uyole, Dk Tulia Ackson  amewahakikishia wananchi  wa Kata ya Iduda Jiji la Mbeya, kuondokana na adha ya maji na mgawo uliopo kufuatia  Serikali  kuja na suruhisho la kudumu la  mradi wa kimkakati  kutoka chanzo cha Mto Kiwira Wilaya ya Rungwe.

Dk Tulia amesema leo Jumatatu  Septemba 29,2025  kwenye mkutano  wa kampeni kuomba kura za wagombea  wa nafasi ya Rais ,wabunge na madiwani  sambamba kueleza  utekelezaji  wa ilani ya uchaguzi 2020-2025.

Amesema  Serikali ilitoa  Sh119 bilioni  kutekeleza ujenzi wa mradi wa maji kutoka  chanzo cha Mto Kiwira  ambao ni miongoni  mwa  miradi iliyomo kwenye ilani ya uchaguzi  2020-2025.

“Ndugu zangu wana Uyole  nyie  mna bahati wakati nipo Mbeya Mjini  mambo mengi nimefanya nikiwa na kata 36 ,lakini kutokana na heshima  kubwa ambayo mlitupa Mimi na Rais Samia Suluhu Hassan  kutupigia kura za kishindo katika Uchaguzi Mkuu  Oktoba  2020 ndio maana tumerejesha  heshima ya kuleta maendeleo,” amesema.

Ametaja baadhi ya miradi iliyopo  katika kata hiyoni pamoja na kupandisha  hadhi shule ya Sekondari  Iduda kuwa na kidato  cha tano na sita,ujenzi  wa mabweni, kisima cha maji na  kupandisha hadhi kituo cha afya Igawilo kuwa Hospitali ya Wilaya.

“Hapa Iduda  CCM, tumerejesha heshima  mlituheshimisha Oktoka 2020 lazima nasi tuwashike mkono  kwa kuleta  maendeleo makubwa,” amesema.

Amesema  Serikali  inakuja na mpango mkakati  wa dira mpya ya elimu ya  mwaka  20/50 itakayo lenga kuboresha  ubora  wa elimu utakaosaidia walimu kuwa mbinu na ufundishaji wanafunzi na sio kukalilisha.

“Yapo mapinduzi na  makubwa yanakuja katika  sekta ya elimu  Serikali  imejipanga kuona  watoto mashuleni hawakalili bali wanaelewa vyema kutokana na ujio  wa  nyenzo na mbinu za ufundishaji,” amesema.

Katika hatua nyingine  amesema  akipata ridhaa watashirikiana na Mamlaka ya Maji Safi  na Usafi  wa Mazingira  Mkoa wa Mbeya (Mbeya Uwsa), kuona namna ya kufunga mabomba ya maji ardhini kusukuma maji kutoka  kisima cha  Shule ya Sekondari  ya Iduda  kuhudumia jamii inayo zunguka,”amesema.

“Wana Iduda Oktoba 29, 2025  tukapige kura mkachague mgombea  urais Samia Suluhu  Hassan na mimi  mbunge  wenu  Dk Tulia  Ackson ili kuwaletea mabadiliko  ya kweli katika nyanya mbalimbali,” amesema.

Amesema Serikali ya  CCM wamejipanga  kufanya  kazi moja ya kufikisha huduma muhimu  kwa Watanzania sambamba na uwekezaji  wa miundombinu  ya majengo  ya mama na mtoto nchi nzima.

Mgombea udiwani Kata ya Iduda, Joseph  Emmanuel amesisitiza kumuomba mgombea ubunge  Uyole,  Dk Tulia kuboresha miundombinu  ya barabara atakapopata ridhaa kuchaguliwa  ili kuwezesha wananchi kusafirisha  mazao na mchanga kutoka maeneo mbalimbali kutokana na miundombinu  mingi kuwa chakavu.