Fyatu kuandamana kuhujumiwa PhD yake

Si juzi viongozi wake wakapiga marufuku tulio na PhD za heshima, kununua, kughushi, na makandokando mengine kutozitumia. Fyatu kama mimi mwenye PhD magunia na uprofesa vya heshima, nikienda kule nikaitwa Daktari au Profesa Emeritus, nafunguliwa mashitaka ya kuhujumu na kudhalilisha elimu na shahada. Nani anazidhalilisha kati ya wanaoziuza au kuzigawa kwa kisingizio cha heshima aka honorarium causa?

Kwa wivu wa viongozi wake kuona tunavyotesa na kukamua kwa kuitwa madaktari si wakaja na huu ufyatu uchwara kwa kupiga marufuku kitu hii wasijue wanatuumiza na kutaka tupate hasara kwa njuluku tulizotumia kununa zana hizi. Sijui kwanini hawajui namna hizi zana zinavyotusaidia kupata ujiko na kisiasa.

Sasa Fyatu nasema wazi. Sifyatuliwi na fyatu yeyote hata awe na mamlaka au kufyatuka kiasi gani. PhD zangu, kwa mfano, nilizinunua tena ka madolari mengi. Hivyo, wanaponipiga marufuku nisifaidi madolari na ujiko huu siyo wizi jamani?

Hii siyo hujuma na ukatili visivyo na mfano? Kwani tumewazuia wao kununua hizi zana na kuzitumia na kufaidi kama tunavyofaidi. Juzi, si Bi Mkubwa aligoma kuniita Daktari. Niliudhika hadi presha ya roho ikanipanda na kuishia kulazwa kwa siku mbili! Hivyo, hawa wanaolenga kutuhujumu wajue wanaweza kutunyotoa roho mbali na kutusababishia usumbufu wa kuonekana kama vihiyo, vilaza, na mbumbumbu wakati tumepata usomi, hata kama siyo kwa kusota darasani, bali kutumia njuluku zetu.

Wakati nijiandaa kuandamana na kususia kupitia kiinchi hiki wakati nikienda zangu majuu nasema yafuatayo: Mosi, nawafyatukia wajue. Kwani kuna ulazima kusomea PhD wakati unaweza kuipata kwa mchoro? Wakati wengine wakisotea hizo shahada, sie tunapiga njuluku za mafyatu na kuzifyatua kwa kutumia kigezo cha heshima hata kama wengine hawana heshima wala elimu achia mbali stahiki hata ya kugusa karatasi zake.

Mbona hawa jamaa wameshindwa kujua kitu kidogo na rahisi kiitwacho kujiongeza na ubunifu? Nani apoteze muda na kuumiza bichwa na bongo wakati kuna njia za mkato? Nani aende kunyanyaswa na maprofesa uchwara wanaojisifia kufelisha wenzao na kutaka kuabudiwa utadhani walipata shahada zao mbinguni?

Kwani hawapo? Nao, nawaonya waache uzwazwa na ukatili huu. Elimu ni haki ya kila fyatu duniani. Kama huna njuluku ya kununua au hujui vilipo vyoo, sorry vyuo vikuu vya mifukoni vinavyofyatua PhD na kuuza shauri yako.

Pili, nasema bila hofu wala woga. Msiingile mambo yetu. Mambo ya Ngoswe muachie Ngoswe na pilipili usiyokula yakuwashani? Acheni wivu wa ki.. we koma! Tusomee tusisomee, tununue, tughushi au tuzawadiwe yanawahusu nini? Acheni tujiongeze, tukamue, tutanue, na kutesa na mwenye wivu akajinyonge au siyo?

Tatu, kama ambavyo kuna mafyatu waliozaliwa hata kujipachika uaskofu kama yule aliyelikoroga wakambwaga, utume, uchunaji, sorry, uchungaji, unabii, nk, pia tupo tuliozaliwa madaktari, mapro, na maprofesa. Mbona kuna madaktari na profesa wa kusomea ambao hawakuelimika zaidi ya kupoteza muda hadi wanajikuta kwenye majalala? Kwani, hawapo jamani?

Nenda kamuulize yule aliyechomolewa kwenye takataka akaishia kuwa mwimbaji kwaya na sifa tena kwa ngurumbili mwenzake. Ni wangapi wanahongwa hata chup ii we koma!

Nne, wakome na kukomaa kabisa na kuacha utoto. Kama hawajui ujiko wa kuitwa daktari bila kusomea waje tuwajuze wajue na kuelewa ili waache uzwazwa na ulimbukeni wa kuingilia madili ya wenzao.

Na kama hawajui zinapopatikana na zinavyopatikana PhD za mchongo na heshima, waje niwape inshu na mbinu waache mbambamba na uvivu wa kufikiri hadi wanatuonea gere madaktari tena bingwa na bobezi kama Dkt Fyatu Mfyatuzi. Ni simpo hivyo.

Tano, najipanga kwenda Umesco kulaani hujuma hii ya kitaalamu. Wakati nikipanga hili, nitahamasisha madaktari wote wa huko wagome kufundisha ili wawafyatue Gen Z wa kule wafanye kama walivyofyatuka wale wa Nepal baada ya kuona picha za vitegemezi na watoi wa wanene wakitanua tena kwa njuluku za umma wakati wao wakitanuliwa na dhiki.

Mwisho, kuonyesha nisivyotania, kuanzia sasa, najiongeza na kujiongezea vyeo vingine. Hivyo, kuanzia sasa naitwa author, hata kama sijaandika hata makala moja. Nitaongeza na sifa ya kuwa expert, specialist, profesa emeritus, daktari, engineer etc wa kufyatuka Fyatu Mfyatuzi esq, sir, nk. Si wamenichokoza wenyewe.

Hawajui kuwa hii ni ngoma kubwa na nzito tena iliyosoma hadi sehemu iitwayo no more class. Kuonyesha ufyatu na usongo wangu, kuanzia sasa, Bi Mkubwa, vitegemezi, hata mifugo yangu itaanza kuitwa madaktari na maprofesa tuone. Mwenye wivu si akajifyatulie mbali badala ya kutuudhi magwiji na wasomi wasio kifani kama mimi. Nyambaff kabisa. Kumbe baa ishafungwa!