Halmashauri Mbarali yatenga Sh900 milioni ununuzi mtambo kukarabati barabara

Mbeya. Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali  Mkoa wa Mbeya,  imetenga zaidi  ya Sh 900 milioni kwa ajili ya ununuzi  wa mtambo mkubwa wa kisasa wa kuchonga miundombinu ya barabara korofi maeneo ya  pembezoni. 

Hatua hiyo imetajwa itakuwa mwarobaini kwa wakulima kuepuka walanguzi na kusafirisha wenyewe mazao kutoka mashambani kuingiza kwenye masoko na kuuza kwa bei nzuri.

Mkurugenzi Mtendaji  wa Halmashauri ya Mbarali,  Raymond  Mweli ameliambia Mwananchi  Digital leo Jumanne Oktoba 7, 2025 wakati akizungumzia mikakati  ya  kuongeza tija ya uzalishaji sambamba  mwarobaini wa kukabiliana  na mabadiliko ya tabia nchi.

“Kwa Wilaya ya Mbarali asilimia 80 ya mapato tunategemea  zao la mpunga  ambapo kwa mwaka wa fedha  uliopita  zaidi ya Sh3.5 bilioni zilikusanywa na kuelekeza kwenye  miradi  mbalimbali  ya maendeleo hususani kuboresha  miundombinu  ya hospitali  ya wilaya, vituo vya afya na zahanati  katika Kata  zote 20,”amesema.

Mweli amesema kutokana na mchango wa sekta ya kilimo, halmashauri  kwa kushirikiana  na Tume ya Taifa ya  Umwagiliaji  imetenga zaidi ya Sh 84.9 bilioni kwa ajili ya ujenzi  wa skimu 100 za  umwagiliaji  kwenye maeneo yenye changamoto  ya maji.

“Lengo  ni kuwaondoa  wakulima na dhana ya kutegemea msimu wa mvua pekee ambayo wakati  mwingine  husababisha athari kutokana na uchache wake kutokidhi mahitaji ya mpunga unaozalishwa,” amasema Mweli.

Amesema mbali na programu ya  ujenzi wa skimu za umwagiliaji, halmashauri  imeweka mikakati  ya pamoja ya  kuwakutanisha  maofisa kilimo na wakulima kuzungumzia  changamoto zinazo wakabilia  katika uzalishaji  na kuzitafutia majawabu.

Katika hatua nyingine Mweli, ametoa maelekezo kwa maofisa kilimo kuanza mara moja kuwaingiza kwenye mfumo rasmi wakulima ili waweze kutambulika, pia kuandika  kwenye mbao za matangazo bei elekezi za pembejeo  za kilimo.

Mkulima wa zao la mpunga Kata ya Rujewa wilayani humo, Steve  Daniel amesema  kitendo cha Serikali  kuboresha miundombinu  ya kilimo cha umwagiliaji  na   barabara kutasaidia wakulima kurejesha matumaini  ya kuongeza  tija katika kilimo hicho.

Amesema changamoto  kubwa kwenye uzalishaji wa zao la mpunga  ni hali ya upatikanaji  wa maji na ubovu muundo  ya barabara jambo  ambalo lilikuwa ni kilio kikubwa ambacho Serikali  imesikia na kukifanyia kazi.