Kiongozi Mbio za Mwenge azindua mradi wa maji Sh705 milioni

Mbeya. Kiongozi  wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa, Ismail Ally Ussi  amesema ameridhishwa  utekelezaji  wa uboreshwaji  na upanuzi wa mradi  wa maji  Kata ya Ipinda Wilaya  ya Kyela Mkoa wa Mbeya,  huku akimtaja Waziri  wa Maji Jumaa Aweso kuiheshimisha Serikali.

Mradi huo wenye thamani ya zaidi  ya Sh705 milioni  utakao hudumia wananchi  10,000 kwa siku ambao unatekelezwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Mbeya (Mbeya -Uwsa), kwa ufadhiri wa fedha za Mfumo waTaifa wa Maji.

Ussi ametoa  kauli hiyo leo Jumamosi  Oktoba 11,2025 wakati akiweka jiwe la msingi kwenye mradi wa maji Kata ya Ipinda Wilaya ya Kyela Mkoa wa Mbeya,  ambao utaondoa adha kwa wananchi na kumtua Mama ndoo  kichwani.

“Wizara ya Maji ni miongoni  mwa wizara  zilizofanikiwa chini ya usimamizi  wa Kaka yetu mweledi Jumaa Aweso kufikisha huduma  ya maji safi na salama kwa wananchi  kwa kushirikiana  na watendaji  wa Mamlaka  ya Maji Mbeya  na wenzetu wa Ruwasa,”amesema.

Amesema katika  mikoa 193 ambayo mbio za mwenge  wa uhuru  kitaifa  umepita  Mkoa wa Mbeya ni miongoni  mwa mikoa ambayo imefanya vizuri katika usimamizi   jambo ambalo limeleta  heshima kubwa kwa Wizara  ya Maji chini ya Serikali ya awamu ya sita.

“Mamlaka ya Maji Mbeya na wenzetu  wa Ruwasa kwa kweli wanaendelea  kuheshimisha Wizara ya Maji naamini ujio wa mwenge wa uhuru  ni ishara ya kuonyesha jinsi gani wana Ipinda wana ondokana na changamoto ya miundombinu ya maji safi na salama,”amesema.

Katika hatua nyingine  ametaja  sababu za ujio wa Mwenge  wa Uhuru ni jambo kubwa na  hakuna mahala uendako  pasipo kuwepo matumaini ,upendo na heshima  baina ya viongozi wa Serikali vyama vya kisiasa na kidini ambao wako kwenye maeneo husika.

“Ni jukumu letu kupitia kauli mbiu ya mwenge  wa uhuru kwa kila Mwananchi   kutimiza wajibu wake kikatiba,kidemokrasia katika taifa hili,lakini kuwakumbusha duniani  hakuna nchi ambayo haiendeshwi kwa mujibu wa katiba na  sheria inayo simamiwa “amesema

 Ussi amesema Tanzania inajivunia katiba ya Jamhuri  ya Muungano ya Tanzania ya mwaka 1977 ibara ya 42 kifungu cha (2) mstari wa 65  inasema Tanzania itaweza kufanya uchaguzi  mkuu kila baada ya miaka mitano.

Amesema  kwa  upande wa Tanzania bara tutaenda kuchagua Rais, wabunge na madiwani na kuomba wananchi wa Ipinda Wilaya  ya Kyela kupitia  hamasa  ya mapokezi  ya mwenge  wa uhuru pia  wajitokeze kwenye uchaguzi  mkuu kumchagua  Rais Samia Suluhu Hassan, wabunge na madiwani .

“Niwatake Oktoba 29,2025  nendeni  mkapige kura kwa wingi katika maeneo yetu twendeni tukamchague Samia tukajenge imani naye  amefanya mambo mengi,lakini wananchi mtarajie   kuona uwepo wa  maboresho  ya miundombinu  ya elimu,afya,maji katika miji na vijijini,”amesema

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji  wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira  Wilaya ya Kyela , Mhandisi  Raphael  Kolong’oyo  amesema  mradi  huo unatekelezwa  na mkandarasi  wa kampuni ya M/s Scorpion  Limited ya jijini  Dar es Salaam.

Amesema mpaka sasa umefikia asilimia 32 na amelipwa Sh222 milioni  kati ya fedha  za mradi  zaidi  ya Sh 705 milioni.

” Awali Kata ya Ipinda  ilikuwa na mradi wa  Kanga group  uliojengwa mwaka 1980 ,lakini baada ya mamlaka kuona ongezeko  la watu  ililazimika kubuni mradi  wa uboreshwaji  na upanuzi  wa huduma ili kukidhi  ongezeko la huduma na upatikanaji  wa rasilimali  hiyo muhimu,”amesema.

Ameongeza uboreshwaji  wa huduma ya maji Ipinda  ulisanifiwa na Mamlaka ya Maji Safi na  Usafi wa Mazingira (Mbeya -Uwsa ), kwa  upande  wa Wilaya  ya Kyela na Kasumuru  mwaka 2022,2023 na kuanza utekelezaji  mwaka 2023, 2024,” amesema.

Amesema  utaondoa  hadha ya upatikanaji  wa huduma ya maji safi na salama ikiwa ni kutekeleza  ilani ya uchaguzi  ya kutaka asilimia 85 ya watanzania  kufikishiwa huduma hiyo  muhimu na kumtua  Mama ndoo kichwani.

Mmoja wa Mama lishe Anitha Elius amesema  wanashukuru  Serikali  kwa kuleta  mradi huo kwani awali walikuwa wakihaha kusaka huduma  hiyo na kununua kwa ndoo  ya lita ishirini kwa Sh500 hadi Sh1,000.