Wakala wa Nishati Vijijini (REA) unaendelea na Kampeni ya kuhamasisha wananchi kuunganishiwa umeme sambamba na kuutumia kujiletea maendeleo.
Kampeni hiyo inafanyika kupitia njia mbalimbali ikiwemo Mikutano ya hadhara na wananchi vitongojini pamoja na kuwatembelea wananchi nyumba kwa nyumba, taasisi kwa taasisi kuwahamasisha, kuwaelimisha hatua na taratibu za kuvuta umeme na elimu ya ulinzi na utunzaji wa miundombinu ya umeme.
Aidha, katika kampeni hiyo kwa nyakati tofauti wananchi wameipongeza REA na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano kwa kila hatua.
Katika kampeni hiyo, wataalam kutoka REA wameambatana na wataalam kutoka Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Mkandarasi, Kampuni ya Sengerema Engineering Group ambaye anatekeleza miradi ya kusambaza umeme katika vitongoji mbalimbali mkoani humo.


