Dodoma. Spika wa Bunge la 13, Mussa Zungu ameahidi kutekeleza mambo matano muhimu katika kuendesha Bunge, ikiwamo kusimamia utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025/50.
Mambo mengine aliyoahidi katika uongozi wake ni uwazi, ushirikiano na kutenda haki kwa vyama vyote vyenye uwakilishi ndani ya Bunge na kusisitiza kuwa, ofisi yake itakuwa wazi kwa kila mbunge kumfikia.
“Nitaongoza kwa kufuata kanuni za Bunge, haki kwa wabunge kutoka vyama vyote, nitakuwa muwazi na kufanya ofisi yangu iweze kufikiwa na kila mbunge atakaponihitaji,”amesema Zungu.
“Kipekee nakushuruku sana Dk Tulia Ackson, ulinilea na kunifundisha kazi, na mimi naahidi kuwa wale watakaochaguliwa akiwamo naibu spika na wenyeviti, tutashirikiana kwa dhati katika kutoa haki.”
Zungu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) amechaguliwa leo Jumanne Novemba 11, 2025 baada ya kupata kura 378 kati ya kura 383 zilizopigwa huku tatu zikiharibika.
Wagombea wengine ni Veronika Tyeah (NLD), Chrisant Ndege (DP) na Amir Yango (ADC) ambao kila mmoja hakupata kura huku Anitha Mgaya (NLD) na Ndonge Said wa AAFP kila mmoja alipata kura moja.
Zungu ambaye ni mbunge wa Ilala jijini Dar es Salaam anakuwa Spika wa sita tangu kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa na uchaguzi mkuu wa kwanza ulifanyika mwaka 1995 Spika wa kwanza alikuwa Pius Msekwa.
Spika wengine waliofuata na kudumu kwa muhula mmoja mmoja ni Samuel Sitta, Anne Makinda, Job Ndugai, Dk Tulia Ackson na sasa Mussa Zungu.
Ushindi wa Zungu katika Bunge la 13, pamoja na kauli yake ya kuendesha chombo hicho kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Bunge, ikiwamo kusimamia utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa, ni ishara kwamba Bunge hilo litakuwa makini katika kuisimamia Serikali.
Baada ya kuapishwa kuwa Spika wa nane tangu uhuru na ni Spika wa sita baada ya kuanzishwa mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992.
Mbunge huyo mbali na kuwashukuru wabunge na chama chake, ameeleza namna atakavyoongoza Bunge katika kutekeleza mipango iliyoainishwa kwenye Dira ya Taifa ya 2025/50.
Miongoni mwa mambo yaliyoainishwa kwenye dira ni eneo la fursa linalolenga kujenga uchumi unaoongozwa na viwanda na teknolojia, hivyo kuongeza fursa za ajira zenye staha hasa kwa vijana na wanawake.
Kwenye usawa na ujumuishi dira inataka kuwepo kwa jamii yenye maelewano, haki, usawa hususani vijana na watu wenye ulemavu ili waweze kushirkishwa kikamilifu na kunufaika na maendeleo.
Eneo la utawala wa sheria na haki katika kipindi hicho, dira inajielekeza katika kuimarisha utawala bora, uwajibikaji, uwazi na utoaji wa haki kwa wakati na kwa usawa kwa kila Mtanzania.
Kuhusu usawa ameeleza namna atakavyotenda haki kwa kufuata misingi ya kanuni za kibunge huku akikwepa kujibu swali kuhusu kauli aliyokuwa akiitoa mara nyingi akiwa naibu Spika ya jaza ujazwe.
Wakati akijieleza mbele ya wabunge, Zungu aliulizwa swali na mbunge wa Mwibara Kangi Lugola kuhusu kauli ambayo amekuwa akiitumia ya jaza ujazwe kama itaendelea kutumika hata kwenye nafasi ya Spika.
Mbunge mwingine aliyemuuliza swali alikuwa ni Ado Shaibu (Tundulu Kaskazini) ambaye ametaka kujua namna gani Zungu atatumia kuleta umoja na haki kwa wabunge wote.
Ni mtaalamu wa uhandisi wa ndege aliyeingia bungeni tangu 2005 na amehudumu katika nafasi mbalimbali ikiwamo mwenyekiti wa kamati ya mambo ya nje kwa miaka 18.
Amehudumu katika ujumbe wa Tume ya Utumishi wa Bunge (2016-2025), kiongozi wa Bunge la Tanzania katika mikutano ya Umoja wa Mabunge ya nchi za Afrika, Pasifiki na Karibiani na Bunge la Jumuiya ya Ulaya.
Nafasi nyingine alizowahi kushika ni kuwa kiongozi wa chama cha Jumuiya ya Mabunge ya Madola Tanzania na mwakilishi wake katika vikao vya kimataifa vya jumuiya hiyo na nafasi kabla ya kuwa Spika, alikuwa Naibu Spika katika Bunge la 12 (2022 hdai 2025).
Kwa mara ya kwanza katika historia ya Bunge la 13, wabunge wameapa kiapo cha uzalendo baada ya kula kiapo cha utii wa Bunge, ambacho kwa kawaida wamekuwa wakiapa kila wanapoingia bungeni kwa mara ya kwanza.
Wabunge kwenye kiapo cha utii kila mmoja aliapa hivi: “Mimi…. naapa kwamba nitakuwa mwaminifu kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kuitumikia, kwa moyo wangu wote na kwamba nitailinda nitaihifadhi na kuitetea Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mujibu wa sheria iliyowekwa, ewe Mwenyezi Mungu nisaidie.”
Huku kiapo cha Spika kikiwa: “Mimi…naapa kwamba nitaitumikia vema na kwa moyo thabiti Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kazi zangu kama Spika wa Bunge na katika kutimiza wajibu wa cheo hicho, nitawatendea haki watu wote kwa mujibu wa Katiba, kanuni za Bunge na sheria, mila na desturi za Jamhuri ya Muungano na kwa vyovyote vile sitatoa siri za Bunge, ewe Mwenzi Mungu nisaidie.”
Mbunge wa Kasulu Mjini (CCM), Profesa Joyce Ndalichako amesema mwelekeo wa Bunge la 13 utakuwa ni mzuri kwa kuwa, mchanganyiko wa wabunge wazoefu na hawa wapya unatia matumaini kuwa, wanakwenda kusimamia Dira ya Taifa 2025/2050 kikamilifu.
“Humu ndani kuna mchanganyiko mzuri, hili litakuwa Bunge lenye maana kubwa kwa wananchi kwani limejaa mchanganyiko mzuri ikiwamo vijana, wasomi na wazoefu hivyo maendeleo yatakwenda kwa kasi,” amesema Profesa Ndalichako.
Mbunge wa viti maalumu, Cecilia Pareso amesema mategemeo waliyonayo ni makubwa kwa Bunge hili kwani halitakuwa Bunge bubu kama wengine wanavyodhani kutokana na ukweli kuwa, Spika aliyechaguliwa ni mtu sahihi katika kutenda haki.
Pareso amesema kati ya mabunge yatakayopigiwa mfano ni hili Bunge la 13 analoliona kuwa Bunge la kazi, umakini na kuisimamia Serikali kikalifu huku akitaja sifa za uzoefu na uwezo wa Spika kwamba utawafikisha wanapopataka.
“Bunge litakuwa la kazi, litakuwa la mchakamchaka na tunatakiwa kuisimamia kikamilifu ilani ya uchaguzi ya CCM ambayo ndiyo imepewa dhamana ya kuongoza nchi, sitegemei kuwa itakuwa chombo bubu,” amesema Pareso.
Mbunge wa Wawi, Ahmed Juma Ngwali amesema matamanio yake ni kuliona Bunge la mchakamchaka wa kimaendeleo lakini liwe lenye kudumisha umoja, ustawi kwa wananchi na kujali masilahi ya wanyonge.
Ngwali ametuma ujumbe kwa Spika Zungu akimuomba kuwa mwenye kutenda haki kwa watu wote wenye nia na malengo thabiti kwa wananchi wanyonge kwa kuwa, akifanya hivyo ataweka heshima kubwa kwa mhimili huo.
Mbunge wa Kilombero, Abubakar Asenga amesema ili kujipambanua na kuonyesha kuwa wanachapa kazi, angetamani Spika Zungu aliongoze Bunge katika umoja, upendo, utulivu na kujali wanyonge.
“Sisi tunaongozwa na mama baada ya kuondokewa na baba, sasa Zungu anatakiwa kutuponya majeraha haya na kutufanya tuishi vizuri, hayo yote yatafanyika ikiwa atakuwa na utulivu na kutujaali hasa tukiwa na hoja za wanyone, afanye kama anavyofanya mama,” amesema Asenga bila kumtaja mama yupi.
Sultan Mataka amesema kuchaguliwa kwa Zungu ni imani kubwa waliyoionesha wabunge wenzake anayotakiwa kuilinda kwa nguvu zote.
Mataka amesema hakuna njia nzuri itakayowavusha wananchi na kuwaondolewa manung’uniko isipokuwa Bunge likisimama vema na kutimiza wajibu wake unaopaswa, hivyo kiongozi wa Bunge lazima awe mfano mzuri.
Hata hivyo, mbunge huyo amesisitiza wabunge kumpa ushirikiano Spika kwani wasitegemee kupokea mema kutoka kwa kiongozi wao kama wao hawampi wala kumuonesha yaliyomema hasa kwenye ushirikiano.
Zuwena Haji amesema Zungu ni mtu mzoefu kwenye mambo ya Bunge, hivyo hana shaka naye lakini akamuomba apunguze utani anapokuwa kwenye kiti chake kwa kuwa, wakati mwingine amekuwa akiingiza utani.