FYATU MFYATUZI: Ole wao wale mafyatu mamluki waliotufyatua

Kwanza, natuma rambirambi kwa mafyatu waliofyatuliwa bahati mbaya baada ya mafyatu wa ‘kigeni’ aka ‘mamluki’ kukinukisha na kutufyatua na kupotezea sifa ya kisiwa cha imani ya amani, mshikamano, mapendano, na upendo.

Nasikia hawa mafyatu wa kigeni waliua mafyatu wetu wasiopenda mbambamba na kusingizia mageshi yetu hasa ndata wasioweza kuua hata mbu. Wakimkamata, wanamuamuru aruke apotelee mbali. Yupo aliyedai eti kuna utekaji! Nani kawambia?

Wanaotekwa, hutekwa na ‘wageni’ na siyo mafyatu wetu. Ndata na vyombo vyetu vya uhasama, sorry usalama, haviwezi kuruhusu hata auawe atekwe au kupotezwa inzi wetu. Hatuwezi kutekana zaidi ya kutakana na kuhitajiana wala hatuwezi kuchoma au kufyatua mali za mafyatu wenzetu au umma. Hatuchomi hata taka.

‘Wote’ waliouliwa walikuwa mamluki. ‘Hakuna haja’ kuwalilia wakati ‘walijitakia.’ Kadhalika, waliochoma na kuiba ni ‘wageni’ hao hao. Msitusingizie.

Niwaonye tena kwa kinywa kipana na herufi kubwa. Komeni na kukomaa kabla hatujawakomesha, mkatokomea, na kukomea kuzimu. Msituzeee. Shauri yenu. Hatuchezi lijapo suala la amani ya imani.

Yeyote anayepanga kukinukisha, atanuka yeye baada ya kumfyatua na kumzika hata kwenye makaburi yasiyojulikana. Ajue. Hata wale wasiojulikana wanaojulikana, sorry, wasioweza kujulikana, hawapendi uchochezi na uchokozi huu. Walaaniwe wote waliosababisha haya mambo.

Kaya yetu ni ya amani. Msituletee chuki, migongano, na uzushi wenu. Nani kawaambia tuna shida? Najua. Mnatuonea wivu. Ndiyo maana mnatuzulia kila uongo dhidi. Kuna waliongopa eti uchafuzi, sorry, uchaguzi wetu haukuwa huru na wa haki.

Kwanza, unawahusu nini? Ungekuwa hivyo, ‘walioshinda’ wangeshindaje kwa aslimia mia? Wapo walioongopa eti kulikuwa na ndata wengi vituo vya kupiga kura. Ebo! Kuna kosa gani ndata wakitiki, tukaweka, na kuchukua? Kwani, wao si wana kaya?

Hata wangechakachua, inawahusu nini nyinyi? Hamjui kuwa nao wana vyama vyao wanavyovipenda na si kosa kikatiba? Kuna kosa gani ndata kumtumikia na kumchagua amuri mujeshi wao? Si wanaonyesha upendo na mapendano ambayo ndiyo alama ya kaya yetu? Yenu mapondano na chuki.

Nisisitize. Mafyatu wetu hawawezi kuandamana tokana na kujazwa, sorry, kujaa imani ya amani mbali na kutokuwa na miguu ya kuchezea kwenda kuandamana.

Hata uwanyanyase vipi, hawawezi kufanya hivyo. Kabla ya maandamano, hamkusikia mkuu mazeri akisema maandamano yatakuwa ya kwenda kuweka, kutiki, na kuchukua kama ilivyotokea tokana naye kuwa na maono hadi kutabiri matokeo. Wapo wanaodai eti matokeo yalipikwa? Loo! Mlitaka yaokwe au kukaangwa? Wengine waliongopa eti tulizima intanet! Kwanza, hakuna aliyezima intanet bali ilijizima. Pili, nani kawambia kuwa intaneti ni chakula au hewa? Wajue.

Mafyatu si wapenzi wala watumiaji wa intanet kutokana na uchochezi wake. Acha haya. Najua. Tunajua. Wanajua. Wanatuonea wivu.

Wengine walihoji kwanini tuliapishana haraka tena kwenye uwanja wa mageshi? Ebo! Walitaka tuapishane baada ya mwaka tena mbele ya wahuni kama hawa mamluki? Kwani, kazi ya mageshi ni nini kama siyo kupokea amri na kulinda chochote tena bila kupoteza muda kuhoji au kuwaza?

Wanaongopa eti kuna mafyatu wa kaya yetu waliuawa. Komeni. Sie siyo machizi, mahayawani, mataahira, wala makatili kuuana sisi kwa sisi.

Sasa elewa na muamini kama alivyosema mazeri mwenyewe. Waliofyatuliwa wakafa ni mafyatu ya kigeni siyo wetu. Nani awezaye kumuua ndugu yake tena kwenye kaya ya amani?

Hatuna sababu wala shida ya kuandamana au kukinukisha. Kwanza, hatunuki. Pili, tunajivunia na kudumisha amani mshikamano wetu.

Tuna demokrasia ya kupigiwa m,fano na iliyotukuka hadi, kama unapendwa, unashinda kwa asilimia mia.

Tuna mafyatu wasiowahi hata kuua inzi. Hatuna ufisadi, umaskini, wala ujinga wowote unaowafanya wale mafyatu viumbe waliozoea kuandamana hata akiwanyea kunguru. Vijana wetu wote wana ‘ajira zinazolipa.’

Anayebisha aende kwenye miji yetu aone wanavyofaidi kuendesha pikipiki na kupiga njuluku kubwa. Tume wapa uhuru wa kutofuata sheria kwa kukatisha kwenye taa nyekundu hata kuuza bidhaa kwenye sehemu za wenda kwa miguu.

Zaidi ya hapa, unataka nini? Uchumi wetu unakuwa kwa kasi ya ajabu. Sisi pekee ndiyo tuna ‘bilionea’ ukanda huu na tunaovutia wachukuaji, sorry wawekezaji kuliko kaya yoyote na tuanochaguana bila kujali viwango vya elimu wala ujuzi.

Eleweni. Tutailinda amani na mshikamano hata kama itahitaji kumwaga damu ya hawa mafyatu wa kigeni. Kwanza, nani kawambia? Sie siyo mazwazwa tuuane sisi kwa sisi. Sisi sote ni ndugu. Hatuna uchama, udini, ukabila, ueneo, ujimbo, wala chuki baina yetu.

By the way, kuna mafyatu waliwafyatua wasanii wetu kuwa ni wasanii na waongo, woga, na machangu! Kwani, kazi yao ni nini? Kuna mbwa walijiita simba.

Kiliponukishwa kikanuka, wakarudia uumbwa wao. Uliona wapi murume akatoga masikio au kuvaa hereni na kuwa na uso kama mwananke akabaki kuwa mrume siyo buabua? Nimesemaje?