TAASISI YA ELIMU TANZANIA (TET) YASHIRIKI MAONESHO YA KIMATAIFA YA VITABU TANZANIA

Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) inashiriki katika maonesho ya Kimataifa ya Vitabu Tanzania,yanayofanyika katika Viwanja vya Maktaba kuu ya Taifa jijini Dar es Salaam.

Maonesho hayo yalianza tarehe 21 Novemba na yanatarajiwa kumalizika tarehe 26, Novemba 2025, ambapo taasisi na mashirika mbalimbali ya ndani na  nje ya nchi  yamejitokeza kushiriki. 

Katika maonesho hayo TET, imetoa elimu kwa wadau mbalimbali waliotembelea katika banda hilo hususani maboresho ya mtaala yanayotekelezwa kwa sasa shuleni katika ngazi ya awali, msingi, sekondari na elimu ya ualimu

Mkuza Mtaala wa Taasisi ya Elimu Tanzania, Bw. Christian Kivenule akizungumza katika maonesho hayo, amesema kuwa utekelezaji wa mitaala unaendelea kwa sasa na kuwaomba wazazi/walezi kuendelea kuwa chanya katika utekelezaji wa mtaala huo.

“Mtaala uliobreshwa uko kwenye utekelezaji na umepokelewa vyema shuleni hivyo tunaamini kuwa mwananfunzi atakapomaliza elimu yake ataweza kupata ujuzi utakaomwezesha kujiajiri na kuajiriwa”amesema Bw. Kivenule.

Aidha Bw. Kivenule amesema kuwa maonesho hayo ya vitabu yametoa fursa njema kwa TET kuendelea kujitangaza zaidi na kufikia wananchi wengi na kuwaomba waendelee kununua vitabu vya kiada na machapisho mbalimbali yanayotumiwa na wanafunzi shuleni kwa sasa ili kujisomea zaidi na kupata elimu na maarifa.

Maonesho hayo yameandaliwa na Chama cha Wachapishaji Tanzania (PATA).