MATEMBEZI Maalumu ndani ya Hifadhi ya Misitu ya Mazingira Asilia Magamba (Magamba Forest Walkathon and Andventure Season 111) yenye lengo la kutangaza na kuhamasisha utalii zinatarajiwa kufanyika Desemba 17 -20 katika mji wa Lushoto mkoani Tanga huku maandalizi yakielezwa kukamilika kwa asilimia 85.
Akizungumza na Mtandao huo Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Misitu ya Mazingira Asilia Magamba, Christoganus Vyokuta amesema kwamba kuelekea mbio hizo wadau mbalimbali wa uhifadhi na utalii watapata fursa ya kujitangaza na kuonesha huduma na bidhaa zao mjini Lushoto.
Alisema kilele cha mbio hizo kitafanyika Desemba 20 ambapo washiriki watashiriki katika matembezi maalumu ndani ya Hifadhi ya Misitu ya Magamba ikiwa ni sehemu ya kutangaza pia vivutio vya utalii vilivyopo ndani ya hifadhi ya Mazingira Asilia ya Magamba wilayani humo
Mhifadhi huyo alisema pia lengo jingine la mbio hizo za Magamba Forest Walkathon and Adventure Season III ni kuunga mkono juhudi za Serikali katika uhifadhi wa mazingira na kukuza utalii ikolojia ikiwemo kuhamasisha Watanzania kutembelea vivutio vya asili vilivyopo nchini.
Mhifadhi huyo amewataka wananchi na wadau wa sekta ya utalii kujitokeza kwa wingi kushiriki katika mbio hizo huku akisisitiza kuwa ushiriki wao ni muhimu katika kulinda rasilimali za asili na kuhakikisha uhifadhi endelevu kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.