Dkt. Abbasi: Watalii Waongezeka kwa asilimia 9 Tanzania

 *Aalika Wananchi Kutalii XMas, Mwaka Mpya Sabasaba Dar

Na Mwandishi Wetu

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii. Dkt. Hassan Abbasi amesema hali ya utalii nchini iko imara kuliko wakati wowote katika historia ya sekta hiyo.

Dkt. Abbasi ameyasema hayo leo Disemba 24, 2025, jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi wa habari mara baada ya kutembelea na kuzindua Maonesho Maalum ya Wanyama yanayoratibiwa na Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA) yaliyoanza Disemba 20 na yataendelea hadi Januari 5, 2026 katika Viwanja vya Sabasaba, Dar es Salaam. 

“Kwanza nianze kwa kuwathibitishia kuwa msisikilize maneno ya pembeni, hali ya utalii nchini iko imara kuliko mtu anavyodhani ambapo tumeona kwa takwimu za Januari hadi Novemba mwaka huu idadi ya watalii wa kimataifa wanaokuja nchini imeongezeka kwa asilimia 9 na ni kubwa zaidi kuliko wakati wowote huko nyuma.

“Takwimu hizo pia zinaonesha idadi ya watalii kutoka nje kwa kipindi hicho mwaka huu ikilinganishwa na mwaka jana imeongezeka kwa takribani watalii 173,000 ikionesha licha ya changamoto mbalimbali duniani sekta hii nchini bado iko himilivu,” alisema Dkt. Abbasi. 

Maonesho hayo yanayofanyika kila siku Viwanja vya Sabasaba mamia ya wananchi wameanza kujitokeza kuona simba, tembo, duma, fisi, nyumbu, ngiri (kasongo) na wanyama wengine wengi.

“Maonesho haya yapo kila siku kuanzia asubuhi mpaka jioni kwa kiingilio rafiki kwa wananchi ambapo watu wazima watalipa Sh. 4,000 na watoto zaidi ya miaka mitano Sh. 1,000 na wale chini ya hapo ni bure,” amesema Kaimu Kamishna Mkuu wa Tawa, Mlage Kabange.