MAFUNZO UFUATILIAJI, TATHMINI KUONGEZA TIJA UTEKELEZAJI WA MIPANGO YA WIZARA

Na Augustina Makoye, WMJJWM – Dodoma

Mkurugenzi wa Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Daktari Hango amesema mafunzo ya ufuatiliaji na tathmini yatawasaidia Maafisa viungo wa ufuatiliaji na tathmini kuelewa kwa kina dhana, taratibu na majukumu ya Ufuatiliaji na Tathmini.

Hango ameyasema hayo akifungua mafunzo ya siku mbili kwa maafisa hao yanayofanyika Desemba 29 na 30, 2025 jijini Dodoma.

Amesema umuhimu wa mafunzo hayo pia ni kupima kiwango cha utayari wa utekelezaji wake katika mipango mikakati na miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Wizara.

“Mafunzo haya yamekuwa jukwaa muhimu la kubadilishana uzoefu na kuimarisha ushirikiano kati ya Maafisa Viungo wa ufuatiliaji na tathmini, hatua itakayosaidia kuimarisha uratibu wa shughuli za Ufuatiliaji na Tathmini katika ngazi zote za Wizara” amesema Hango.

Aidha, amesema kuwa washiriki watakuwa kwenye nafasi nzuri ya kutambua changamoto ili wizara iweze kuzipatia ufumbuzi mapema, kupima mafanikio ya miradi ya maendeleo kama imeleta mabadiliko chanya au athari kwa walengwa, pamoja na kuongeza ufanisi wa kuhakikisha rasilimali zinatumika kwa njia bora na yenye matokeo makubwa.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Mipango Wizarani hapo Sifuni Ombeni amekipongeza kitengo cha Tathmini na Ufuatiliaji kwa kuandaa mafunzo haya ambayo yatakuwa na tija katika uandaaji wa bajeti na maandiko mengine ya Wizara.

Mafunzo hayo yanatolewa na mtaalamu mwelekezi Herbert Maximilian Lyimo, Afisa Mkuu Ufuatiliaji na Tathmini kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu – Sera, Bunge, Uratibu na wenye Ulemavu; Idara ya Ufuatiliaji na Tathmini ya Utendaji wa Serikali (DPME).