TANESCO RUVUMA YAHIMIZA MATUMIZI YA VIFAA VYA UMEME VYENYE UBORA MAJUMBANI KUEPUKA HATARI

Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa TANESCO mkoa wa  Ruvuma, Alan Njiro, ametoa wito kwa wateja wa shirika hilo kuhakikisha wanatumia vifaa vya umeme vyenye ubora na vinavyokidhi viwango katika nyumba zao ili kuepuka changamoto na hatari zinazoweza kujitokeza kutokana na matumizi ya vifaa visivyo na ubora au feki.

Njiro ametoa wito huo akiwa katika Mtaa wa Pambazuko, Kata ya Shule ya Tanga, Manispaa ya Songea Mkoani Ruvuma, wakati akitoa elimu kwa wananchi waliopitiwa na Mradi wa REA Awamu ya Pili, amehimiza wananchi kununua vifaa vyenye alama za ubora na kutumia mafundi waliosajiliwa na wenye ujuzi wakati wa kusuka miundombinu ya umeme katika nyumba zao.

Kwa upande wake, Afisa Usalama wa TANESCO Mkoa wa Ruvuma, Paulo Maysoli, amewataka wananchi wa mkoa huo kutunza na kuilinda miundombinu ya umeme dhidi ya uharibifu na vitendo vya wizi, akisisitiza kuwa miundombinu hiyo ni mali ya umma na ni jukumu la kila mwananchi kuilinda na kuitunza.

Aidha, wananchi wa Mtaa wa Pambazuko wameishukuru Serikali kwa kuwapelekea mradi wa REA katika mtaa wao, wakieleza kuwa mradi huo utachangia kuboresha maisha yao na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii.

TANESCO Mkoa wa Ruvuma imewahimiza wananchi kushirikiana na taasisi husika kwa kuzingatia matumizi ya vifaa vya umeme vyenye ubora, kuzingatia ushauri wa kitaalamu na kulinda miundombinu ya umeme, ili kuhakikisha usalama, uendelevu wa huduma ya umeme na maendeleo endelevu katika jamii.