Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Laurent Deogratius Luswetula, alifanikiwa kutembelea banda la HaloPesa wakati wa Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa, yaliyofanyika katika Viwanja vya Usagara, mkoani Tanga, na kupata fursa ya kujionea pamoja na kuelimishwa kuhusu huduma mbalimbali za kifedha zinazotolewa na mtoa huduma huyo wa kifedha kidijitali.
Akiwa katika banda hilo, Mhe. Luswetula alizungumza na Mkuu wa Idara ya Biashara wa HaloPesa, Bi. Happy Mzena, ambaye alimueleza kuhusu mchango wa HaloPesa katika kukuza ujumuishaji wa kifedha nchini, hususan kwa kuwafikia wananchi waliopo maeneo ya vijijini, wafanyabiashara wadogo na wa kati, pamoja na makundi yenye uhitaji maalum wa huduma rahisi na salama za kifedha.
Mhe. Luswetula aliipongeza HaloPesa kwa kuendelea kubuni na kutoa huduma za kifedha zinazotumia teknolojia ya kidijitali, ambazo zimekuwa chachu ya kurahisisha miamala ya kifedha, kupunguza gharama za huduma, na kuongeza usalama wa fedha kwa wananchi. Aidha, alisisitiza umuhimu wa wadau wa sekta ya fedha kushirikiana na Serikali katika kufikia malengo ya Taifa ya ujumuishaji wa kifedha na uchumi wa kidijitali.
Kwa upande wake, Bi. Happy Mzena alisema kuwa HaloPesa inajivunia kuwa sehemu ya safari ya maendeleo ya sekta ya fedha nchini kwa kushirikiana na Serikali na wadau wengine katika kutoa suluhisho za kifedha zinazokidhi mahitaji ya wananchi wa rika na makundi mbalimbali. Aliongeza kuwa HaloPesa itaendelea kuboresha huduma zake ili kuhakikisha Watanzania wengi zaidi wanapata huduma za kifedha zilizo rahisi, salama na zinazopatikana kwa wakati.
Maadhimisho ya Wiki ya Huduma za Fedha Kitaifa yanalenga kuongeza uelewa kwa umma kuhusu umuhimu wa huduma za kifedha, matumizi ya teknolojia katika sekta ya fedha, pamoja na kuhimiza wananchi kushiriki kikamilifu katika mfumo rasmi wa kifedha kwa ajili ya maendeleo ya mtu binafsi na Taifa kwa ujumla.
HaloPesa Tumerahisisha, Kwa makato nafuu zaidi!


