Dar es Salaam. Tofauti na matarajio ya wengi waliokuwa wakikosoa na kuhofia iwapo Bunge la 13 lisingeweza kuweka mbele maslahi ya wananchi katika kusimamia uwajibikaji wa Serikali kutokana na kutawaliwa na chama kimoja, hali inaonekana kubadilika.
Tangu kuanza kwa Mkutano wa Pili wa Bunge la 13 unaoendelea jijini Dodoma, baadhi ya wabunge wameibua hoja nzito zilizogusa masuala nyeti ya uwajibikaji, utawala bora na mapambano dhidi ya ufisadi.
Miongoni mwa wabunge walioibua hoja zilizozua mijadala katika mitandao ya kijamii ni wa Mwibala, Kangi Lugola pamoja na Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabiby.
Hoja zao zimeonekana kupingana na hofu ya awali ya baadhi ya wananchi kuhusu uwezo wa Bunge hilo kuisimamia Serikali kwa ufanisi.
Akichangia mjadala bungeni Alhamisi, Januari 29, 2026, wakati akizungumzia maono ya Rais Samia Suluhu Hassan ya kuijenga Tanzania mpya kama yalivyoainishwa katika hotuba yake ya ufunguzi wa Bunge la 13, Mbunge Lugola alikemea vikali kile alichokiita ‘uchawa’, akieleza kuwa ni hatari kwa maendeleo ya Serikali.
“Tuboreshe eneo moja ambalo tusipolishughulikia litakwaza mipango ya Serikali—machawa. Ndani yake ndimo wanamojificha mafisadi na wabadhirifu. Bila kukiteketeza na kukiondoa kichaka hiki, mipango ya Serikali haitafanikiwa,” alisema mbunge huyo.
Aidha, alisisitiza umuhimu wa kuimarisha misingi ya utawala kwa kuhakikisha mihimili ya dola, ambayo ni pamoja na Bunge, Mahakama na Serikali, inafanya kazi kwa uhuru.
“Tunapoletewa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ni lazima tuwe huru ili kushughulikia wabadhirifu na maazimio yetu yaheshimiwe,” aliongeza.
Pia, alitaka vyombo vya dola viwe huru, akisisitiza kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) anapaswa kuwa huru ili mafisadi wachukuliwe hatua za kisheria, huku Jeshi la Polisi likitakiwa kuwapa askari wake uhuru wa kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria badala ya maelekezo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Gairo, Ahmed Shabiby, alipokuwa akimpongeza Waziri Mkuu, Dk. Mwigulu Nchemba, bungeni hapo, alisema ameanza vyema majukumu yake, lakini akakiri kuwa ufisadi bado ni tatizo kubwa linalotambuliwa hata na wananchi.
“Naomba Waziri Mkuu muangalie haya yanayoendelea. Wananchi wa sasa si wajinga, wanaelewa kila kinachoendelea. Wanaona kabisa majumba ya kifahari ya baadhi ya watu walioko serikalini na kutambua kilicho nyuma yake. Hata mimi nikiombwa naweza kuwataja,” alisema.
Mbali na hoja hizo, Mbunge wa Chemba, Kunti Majala, naye aliibua mjadala uliozua hisia tofauti kwenye mitandao ya kijamii baada ya kuhoji matukio ya Oktoba 29, 2025, akitaka uwajibikaji kwa waliodaiwa kuhusika na mauaji ya watu wasio na hatia.
“Niwaombe Watanzania wenzangu, tuilinde lulu hii tuliyo nayo. Siyo jambo la kuchezea kama kiberiti. Wapo walioathirika bila kuhusika na vurugu hizo, lakini watu wasio na hatia waliangamizwa kwa tamaa zetu binafsi. Tuwaheshimu waliotutangulia kupigania uhuru ili tuweze kujisimamia sisi wenyewe,” alisema, huku akisisitiza umuhimu wa kulinda amani na umoja wa kitaifa.
Hata hivyo, wachambuzi wa masuala ya siasa nchini waliozungumza na Mwananchi kwa nyakati tofauti kuhusu hoja za wabunge hao na mjadala unaoendelea miongoni mwa wananchi, wamesema bado ipo changamoto kwa baadhi ya Watanzania kuwatazama wabunge kwa misingi ya vyama vyao badala ya kutathmini utekelezaji wa wajibu wao wa kikatiba.
Aidha, baadhi ya wachambuzi hao wamegusia kuwa hali hii inayoendelea bungeni inachochewa na joto la uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2030.
Akizungumzia suala hilo, mchambuzi wa masuala ya siasa, Hamduny Marcel, amesema anaiona hatari ya wananchi kupoteza imani kwa mamlaka za Serikali na taasisi zake, akionya kuwa viongozi wanapaswa kupimwa kwa utendaji wao badala ya vyama vyao vya siasa.
“Ipo hatari kubwa iliyojengeka ambapo watu wengi wameanza kupoteza imani kwa Serikali na taasisi zake. Ndiyo maana wengine wanaamini kuwa mpinzani pekee ndiye anayeweza kuibua hoja za msingi. Chuki ya kisiasa imekuwa kubwa, hali iliyosababisha wananchi wengi kuondoa imani yao kwa Serikali na kujenga taswira kuwa mbunge wa chama tawala hawezi kuibua hoja za msingi dhidi ya Serikali,” amesema.
Amesema wabunge huchaguliwa na wananchi kwa jukumu la kusimamia maendeleo ya umma, hivyo jamii inapaswa kuondokana na fikra kwamba wabunge wa chama tawala hawawezi kuibua hoja za msingi.
Amesisitiza umuhimu wa kuwatazama wabunge kwa misingi ya utendaji wao, si kwa itikadi za vyama vyao.
Kwa mtazamo tofauti, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Sabatho Nyamsenda, amesema hoja za wabunge na viongozi wanaoibua mijadala mikubwa ya uwajibikaji zinahusiana kwa karibu na mazingira ya kisiasa nchini pamoja na joto la kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2030.
Nyamsenda ametaja sababu tatu. Kwanza, amesema huu ni muhula wa mwisho wa Rais Samia Suluhu Hassan madarakani, hivyo kila mbunge au waziri anatafuta uhalali na uungwaji mkono wa wananchi kuelekea uchaguzi ujao. Amesema kauli ya Mbunge wa Gairo, Shabiby, kwamba kila mtu anatafakari hatima ya mwaka 2030, inaakisi hali hiyo.
“Pili, kwa mara ya kwanza katika historia ya Tanzania, matukio ya Oktoba 29, 2025 yameonesha kiwango ambacho baadhi ya wananchi wamepoteza imani kwa Serikali. Hivyo, hiki ni kipindi ambacho wanasiasa wengi wanajaribu kujiosha kisiasa kuelekea uchaguzi mwingine,” amesema.
Akitaja sababu ya tatu, Nyamsenda amesema inatokana na mwelekeo wa hali ya kisiasa nchini unaoashiria uwezekano wa kufanyika mabadiliko katika mifumo ya siasa na uchaguzi kutokana na madai na harakati zinazoendelea. Amesema hali hiyo inawafanya wanasiasa kujaribu kwenda sambamba na upepo wa Watanzania ili waendane na mwelekeo wao.
“Ni jambo la kawaida katika awamu ya mwisho ya Rais aliyepo madarakani; hata viongozi waliomo ndani ya Serikali hupunguza kumzingatia zaidi kiongozi huyo na kuanza kujipanga kwa uchaguzi ujao. Huu ni wakati ambao wanasiasa wanaotaka kuendelea kushiriki katika awamu zijazo huibuka na hotuba za kutafuta imani ya wananchi,” ameongeza.