Nadhani wengi mmeishasikia baadhi ya wanandoa walioshindwa kuimarisha ndoa zao kwa sababu mbalimbali wakitafuta misaada.
Si vibaya kutafuta misaada hata ushauri. Je, ni wapi upate vitu hivi na wakati gani na namna gani ufanye hivyo? Nini unapaswa kuzingatia na kutahadhari?
Hili ndilo suala tutakalodurusu leo. Ni jambo la kawaida kusikia wanandoa wakienda kwa viongozi wa dini hasa wachungaji/mashehe kutafuta suluhu ya matatizo ya ndoa zao. Je unapofanya hivyo, huwa umechunguza ndoa zao, uadilifu, ubora, hata uovyo wao kwanza?
Je, ni kila mchungaji ni mchungaji au wengine ni wachunaji na hata wazinzi na wezi wa kawaida wanaoweza kukutumia na kuongeza ukubwa wa tatizo badala ya kulitatua?
Mfano, unakwenda kwa padri. Vizuri. Je, padri, japo amepewa mamlaka ya kufungisha ndoa, je, mambo ya ndoa anayajuaje wakati haoi wala hajaiwahi kuishi na mke ukiachia mbali hawa wenye ndoa fiche?
Unaweza kujitetea kuwa amesomea. Hata akisomea, hawezi kuwa na ujuzi na uzoefu sawa na wanandoa. Hivyo, kwenda kwa mtu kama huyu kunaweza kuwa chanzo cha kuongeza ukubwa wa tatizo.
Wengine huenda kwa waganga wa kienyeji ambao siku hizi wameongezeka sana. Hawa hawana cha maana cha kukupa zaidi ya kukuibia, kukudhalilisha, na kukuongezea tatizo. Huu ni upumbavu wala si ujinga.
Ni sawa na wale wanaokwenda kwa waganga kutafuta utajiri. Kama waganga wangekuwa na uwezo wa kukupa utajiri, inakuwaje walio wengi ni maskini tena wa kunuka? Hawa, hawafai kabisa.
Uzoefu wetu kutokana na utafiti hata kusikiliza yaliyowakuta waliofanya hivi, unatuambia kuwa hawa ni wa kuepuka kama ukoma au Ukimwi. Kwani, wengi ni wababaishaji, wazinzi, na wezi wa kawaida tu.
Wengine huenda kwa mashoga au maraafiki zao. Hata hivyo, kufanya hivyo, nako, kunaweza kukuza tatizo badala ya kulitatua.
Ushaambiwa ndoa ni ya wawili. Je, unaaminije kuwa hawatakuwa nyongeza ya tatizo? Je, unajua matatizo yaliyomo kwenye ndoa zao? Ni nini wanacho ambacho wewe huna? Nini wanaweza wewe huwezi? Jiulize zaidi. Je, wao wanakuamini au kukudharau? Je, wanaaminika au hata kujali?
Wanandoa na watarajiwa wote wajue. Kupata changamoto au matatizo kwenye ndoa siyo mwisho wake. Ni sawa na kuwa mzima na kuugua, kupata na kukosa katika maisha.
Ni mambo yanayokufikirisha na kukupa jitihada, nyenzo, ubunifu, na uvumilivu wa kuyakabili na kuyatatu. Hivyo, inapotokea, unaweza kufanya yafuatayo:
Mosi, utulize mawazo yako ili akili yako isichanganyikiwe na kukushawishi kufanya mambo ambayo si jibu bali tatizo. Unapofanya uamuzi ukiwa na haraka, hofu, au wasiwasi, matokeo yatakuwa mabaya tu.
Pili, kama ni lazima upate msaada, nenda kwa wazazi wako baada ya kujiridhisha wanaweza kukusaidia. Maana, si wazazi wote wanaweza.
Mfano, wazazi waliotalikiana au wenye matatizo walioshindwa katika ndoa yao, hawawezi kukusaidia. Wangekuwa wanaweza, basi wengetatua matatizo yao kwanza.
Tatu, fanya utafiti kwanza ili kujua aina, chanzo, ukubwa wa tatizo ili uweze kujiandaa vilivyo. Hapa ndipo inapokuja hatua ya nne.
Nne, jisomee makala na vitabu vinavyohusiana na ndoa uone kama kuna wenye tatizo kama lao ili kujua lilipotokea, wahusika walifanya nini kulitatua.
Tano, ikizidi ikapungua, mlilie Mungu wako badala ya kujihangaisha na watu ambao nao wanayo yao tena mengine makubwa kuliko yako.
Sita, unaweza kupata msaada kwa mwenzako. Hapa, kama wahusika mtakuwa wakweli, mkishirikiana mtapata chanzo cha tatizo na kutafuta suluhu pamoja.
Ndoa ni kama baiskeli. Kama gurudumu moja kati ya mawili litapata pancha, lililobaki haliwezi kufanya kazi yoyote. Na mara nyingi, matatizo ya ndoa huanzia kwa wanandoa wenyewe iwe kwa hiari au kwa bahati mbaya.
Mnaposhirikiana wawili, kwanza, mtajua chanzo ni nani au nini na mfanye nini. Pili, mtakuwa na vichwa zaidi ya kimoja. Tatu, wote mtajiona kama mko hatarini. Hivyo, mtapambana pamoja badala ya kupambana mmoja dhidi ya mwingine.
Hata katika kudurusu na kufanyia tatizo lenu utafiti, mtagwana maeneo ya kushughulikia mbali na kupeana maoni na ushauri au namna mnavyolielewa, kutolielewa au kuliendea tatizo. Kwenu, huu ni msaada mkubwa.