Tausi yasaka kocha, yupo Chabruma

TAUSI FC inayoshiriki Ligi Kuu ya Wanawake inaangalia uwezekano wa kumpata aliyekuwa kocha wa zamani wa JKT, Ester Chabruma.

Tausi imetoka mkiani na kusogea hadi nafasi ya saba kwenye msimamo wa ligi ikiwa na pointi 11, imeshinda mechi nne, sare mbili na kupoteza tano.

Timu hiyo imefanya maboresho dirisha hili ikimpa mkono wa kwaheri kocha mkuu, Gustavo Adolfo raia wa Mexico pamoja na kocha wa utimamu wa mwili, Joseph Mapembe ikimuaga mapema wiki iliyopita.

Kocha huyo aliitumikia Tausi mzunguko wa kwanza kwenye mechi 10 alipata ushindi nne, kupoteza nne na sare mbili.

Chanzo kililiambia Mwanaspoti timu hiyo imeanza msako wa kutafuta kocha mpya wa ndani na nje na miongoni mwao jina la Chabruma lipo.

Kiliongeza kama hawatampata kocha kutoka nje basi huenda Chabruma akapewa mkataba wa muda kukiongoza kikosi hicho hadi watakapompata kocha wanayemhitaji.

“Wapo makocha wengi ambao wanawatazama wa nje na ndani lakini shida ni pesa, hivyo kama ofa hazitawashawishi makocha wanaozungumza nao basi watamkabidhi timu Chabruma hadi mwisho wa msimu angalau kumalizia ligi,” kilisema chanzo hicho.

Chabruma ambaye ni mshambuliaji wa zamani wa timu ya taifa ya Wanawake, Twiga Stars aliachana na JKT msimu wa 2024/25 baada ya kuipa ubingwa wa ligi, ubingwa wa ngao ya jamii na kombe la Michuano ya Afrika Mashariki na Kati kufuzu Ligi ya Mabingwa Afrika.