BAADA ya kukosa ushindi kwenye mechi tano mfululizo za Ligi Kuu Bara, uongozi wa Mashujaa upo katika mazungumzo ya kumalizana na kocha wa kikosi hicho, Salum Mayanga ili kufikia makubaliano ya kuvunja mkataba.
Hatua hiyo inakuja ikiwa ni baada ya timu hiyo kuchapwa bao 1-0 na KMC, kwenye Uwanja wa Majaliwa mkoani Lindi, Februari 3, 2026, kikiwa ni kichapo cha tatu mfululizo, ingawa ni mechi ya tano ya Ligi Kuu bila ya kuibuka na ushindi.
Katika mechi tano zilizopita za timu hiyo katika Ligi Kuu Bara, Mashujaa imetoa sare mbili na kuchapwa tatu, huku mara ya mwisho kushinda ilikuwa ni pale ilipoilaza Mbeya City bao 1-0 Novemba 22, 2025, jambo linalotishia kusitishiwa mkataba wake.
Taarifa kutoka ndani ya uongozi wa timu hiyo, imeliambia Mwanaspoti baada ya mechi ya KMC, Mayanga alipewa maelekezo ya kuandika barua ya kueleza sababu inayochangia mwenendo huo, japo uamuzi wa kumsitishia mkataba wake uko hatua za mwisho.
“Uamuzi wa kuachana naye ulifanyika na hata mechi na KMC ilikuwa ni kipimo cha mwisho kwake cha kujitetea, nadhani muda wowote kuanzia sasa makubaliano ya kuachana yatafikiwa ili kila mmoja aangalie changamoto mpya,” kilisema chanzo hicho na kuongeza:
“Haturidhishwi na matokeo, timu inapitia nyakati ngumu, hatuelewi shida ni nini, hivyo kama uongozi tumekubaliana cha kufanya ili kutuliza presha iliyopo.
“Kocha ndio muda mwingi anakaa na wachezaji anaweza kufahamu nini kinasababisha shida iliyopo sasa, lakini pia kufahamu yeye pia anachukua uamuzi gani kutokana na changamoto iliyo mbele yetu hasa hii ya matokeo mabaya, mechi tano mfululizo tumekusanya pointi mbili.”
Mayanga alijiunga na Mashujaa FC Machi 21, 2025, akitokea Mbeya City, akienda kuchukua nafasi ya kocha, Abdallah Mohamed ‘Baresi’, ikiwa ni muda mfupi baada ya kikosi hicho kuchapwa mabao 3-0 na Singida Black Stars, Februari 26, 2025.
Kocha huyo wa zamani wa Mtibwa Sugar, msimu huu ameiongoza Mashujaa katika mechi 12 za Ligi Kuu, ambapo kati ya hizo ameshinda tatu, sare nne na kupoteza tano, ikifunga mabao matano na kuruhusu 13, ikiwa nafasi ya 10 kwa pointi 13.
Mwanaspoti lilimtafuta Ofisa Habari wa Mashujaa, Steven Ndorobo ambaye amesema bado wana nafasi ya kurekebisha makosa yao katika michezo ijayo, huu sio wakati wa kuikatia timu tamaa.
“Ni kweli tumepoteza mchezo wa tatu mfululuzo, lakini tunayo michezo mingine 18 mbele yetu ya kujisahihisha, huu sio wakati wa kulaumiana. Viongozi wanaona pia kinachoendelea na wanajua, na tunaumizwa pia na matokeo haya lakini ndio mpira.
“Tunautazama mchezo unaofuata dhidi ya Tanzania Prisons tunaokwenda kucheza Mbeya, timu imeshaanza safari ya kuwafuata wapinzani na tupo sambamba na kocha, yanayoendelea ni porojo tu,” amesema Ndorobo.
