Kakama kutathmini mafanikio miaka 10 ya Kiswahili Jumuiya ya Afrika Mashariki Zanzibar

Dar es Salaam. Wanajumuiya ya Afrika Mashariki wanatarajiwa kukutana kwenye maadhimisho ya miaka 10 ya Kamisheni ya Kiswahili Afrika Mashariki (Kakama) ambapo itafanyika tathmini na kujadili mustakabali wa lugha ya Kiswahili kwa miaka ijayo.

Maadhimisho hayo yatakayowakutanisha wadau mbalimbali na wananchi kutoka nchi nane za Jumuiya ya Afrika Mashariki, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Kenya, Rwanda, Somalia, Sudan Kusini, Uganda na Tanzania yamepangwa kufanyika Februari 14, 2026 mjini Zanzibar.

Akizungumza leo Ijumaa Februari 6, 2026, katika kipindi cha Kiswahili cha Rula kinachorushwa kupitia UFM, Dk Caroline Asiimwe amesema maadhimisho hayo yatawakutanisha wadau mbalimbali wa Kiswahili na viongozi mbalimbali ili kutathmini na kujadili mustakabali wa lugha hiyo.

Amesema miongoni mwa mafanikio ya Kiswahilili katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ni pamoja na kutumika kama lugha rasmi ya jumuiya na nchi zingine kutumia kama lugha yao ya Taifa, zingine zikitumia kama lugha ya pili pamoja na mawasiliano rasmi.

Dk Asiimwe amesema katika kikao cha 21 cha wakuu wa nchi za Afrika Mashariki waliazimia Kiswahili kutumika kama lugha rasmi ya mawasiliano ndani ya jumuiya hiyo jambo ambalo limeifanya pia lugha hiyo kutumika kama nyenzo ya kuchochea uchumi.

Amesema Kakama imekuwa ikishirikiana mabaraza ya Kiswahili ya nchi wananchama na mamlaka husika ili kutekeleza majukumu yake, huku akihimiza nchi zingine wananchama kukahikisha kuhakikisha wanaanzisha mabaraza hayo.