Urusi imefanya shambulizi kubwa dhidi ya miundombinu ya nishati nchini Ukraine, hatua iliyosababisha kukatika kwa umeme katika maeneo mengi ya nchi hiyo. Taarifa hiyo imetolewa leo na Kampuni ya Taifa ya Umeme ya Ukraine, Ukrenergo.
Kupitia ujumbe uliotolewa kwenye mtandao wa Telegram, Ukrenergo imesema kuwa mashambulizi hayo bado yanaendelea, huku ikibainisha kuwa shughuli za kurekebisha miundombinu iliyoharibiwa zitaanza mara tu hali ya usalama itakapoimarika.
Waziri Mkuu wa Ukraine, Denys Shmygal, amesema serikali ya Kyiv imeomba msaada wa dharura kutoka Poland kufuatia mashambulizi ya Urusi yaliyolenga vinu vya kuzalisha umeme vya Burshtynska na Dobrotvirska, vilivyopo magharibi mwa Ukraine.
Maafisa wa Ukraine wameishutumu Urusi kwa kulenga kimakusudi miundombinu ya nishati, mashambulizi ambayo yamesababisha kukatika kwa umeme na kuwaacha mamia ya maelfu ya raia bila huduma ya umeme katika kipindi hiki kigumu cha msimu wa baridi.
Related
