MKUTANO Maalumu wa 59 wa Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) umeanza katika Makao Makuu ya Jumuiya jijini Arusha, ikiwa ni maandalizi ya Mkutano wa 25 wa Wakuu wa Nchi Wanachama wa Jumuiya hiyo unaotarajiwa kufanyika tarehe 7 Machi 2026 jijini Arusha.
Mkutano huo Maalumu wa 59 wa Baraza la Mawaziri umeanza katika ngazi ya Wataalamu kuanzia tarehe 2 hadi 3 Machi 2026, ambapo katika hatua hiyo Wataalamu watapitia na kujadili agenda na taarifa mbalimbali zitakazowasilishwa na kujadiliwa katika mkutano wa ngazi ya Makatibu Wakuu tarehe 4 Machi 2026 na hatimaye ngazi ya Mawaziri unaotarajiwa kufanyika tarehe 5 Machi 2026.
Miongoni mwa masuala yatakayojadiliwa katika mkutano huo ni pamoja na kupokea na kujadili; ripoti ya Mwaka ya Baraza la Mawaziri la Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa kipindi cha tarehe 30 Novemba 2024 hadi 30 Disemba 2025, ripoti ya Baraza la Mawaziri wa Jumuiya kuhusu Utekelezaji wa Maamuzi na Maelekezo ya Mikutano iliyopita ya Wakuu wa Nchi za EAC, uzinduzi wa Mkakati wa Saba wa Maendeleo wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (2026/27 – 2030/31) na uzinduzi wa Dhamana ya Forodha ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC Customs Bond/Guarantee).
Vilevile, mkutano huo utajadili kuhusu; zoezi la kuridhia na kusaini kwa Miswada ya Sheria zilizopitishwa na Bunge la Afrika Mashariki, uteuzi wa Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, kuhuisha Mkataba wa Uteuzi wa Naibu Makatibu Wakuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, uteuzi wa Majaji wa Mahakama ya Jumuiya na utoaji wa zawadi kwa Washindi wa Uandikaji wa Insha.
Ujumbe wa Tanzania katika mkutano huo unaongozwa na Bw. Benjamin Mwesiga, Mkurugenzi wa Biashara, Uwekezaji na Sekta za Uzalishaji katika Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ukijumuisha wajumbe kutoka Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi na Utawala Bora; Ofisi ya Rais- Mipango na Uwekezaji, Wizara ya Fedha; Wizara ya Viwanda na Biashara na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Jumuiya ya Afrika Mashariki ina nchi wanachama nane, ikiwa na idadi ya zaidi ya watu milioni 300 na pato la pamoja linalokadiriwa kuzidi dola za Marekani bilioni 300, hali inayoifanya Jumuiya hiyo kuwa miongoni mwa Jumuiya za kikanda zenye soko kubwa na fursa lukuki za uwekezaji barani Afrika.
.jpg)



.jpg)