Na Neema Adrian
Kampuni ya Bia ya Serengeti (SBL) jana ilikutana na Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, katika kikao cha kimkakati kilicholenga kuimarisha mnyororo wa thamani wa kilimo nchini, kuwawezesha wakulima na kuchangia maendeleo ya viwanda na uchumi wa Tanzania.
Wawakilishi wa SBL walikuwa ni Mwenyekiti wa Bodi, Paul Makanza na Mkurugenzi Mtendaji, Obinna Anyalebechi ambao waliongoza mazungumzo hayo.
Mwenyekiti wa Bodi alimpongeza Chongolo kwa kuteuliwa na kusisitiza dhamira ya muda mrefu ya Kampuni ya Bia ya Serengeti ya kuunga mkono ajenda ya Serikali ya mapinduzi ya kilimo na viwanda kupitia uwekezaji endelevu na ushirikiano na sekta binafsi.
Kampuni ya Bia ya Serengeti imejikita katika kuendeleza kilimo na viwanda kupitia uwekezaji thabiti na ushirikiano wa muda mrefu na serikali.
Katika muktadha huo, maafisa wa SBL walimueleza Waziri Chongolo juu ya ongezeko la uwekezaji wa kampuni hiyo katika kilimo cha ndani.
Mwaka mwaka 2024, SBL ilinunua takriban tani 20,000 za nafaka nchini, zikifanikisha zaidi ya 80% ya mahitaji yake ya mwaka ya malighafi.
Uuzaji huo wa ndani unasaidia kupunguza utegemezi wa ununuzi wa malighafi nje na kuimarisha minyororo ya usambazaji nchini huku ukisaidia wakulima wa Kitanzania.
Kwa wakulima wa shayiri, mahindi na mtama mazao yanayosaidia uzalishaji wa bia, SBL inachangia kukuza ajenda ya viwanda Tanzania.

Kila mwaka, kampuni inachangia zaidi ya shilingi bilioni 15 kwa wakulima walioko katika minyororo yake ya kilimo.
SBL pia ilizundua mpango wake wa “Shamba ni Mali” mwaka 2025, ambao unalenga kuongeza tija ya wakulima na kukuza soko la wakulima nchini.
Kupitia mpango huu, kampuni inashirikiana na wakulima zaidi ya 600 wanaolimisha shayiri, mahindi na mtama, ikiwapa mafunzo ya kilimo, pembejeo na mbinu za kilimo zinazoongeza afya ya udongo, kuongeza mazao na kusaidia kilimo kinachoendana na mabadiliko ya tabianchi.
Mpango huo ni jumuishi na unalenga kusaidia wanawake wakulima na watu wenye ulemavu, kuhakikisha kwamba faida za kilimo zinawafikia wote.
Kupitia mpango wake “Kilimo Viwanda”, SBL pia imewekeza katika kizazi kipya cha wataalamu wa kilimo.
Mpango huo umeunga mkono zaidi ya vijana 300 wa Kitanzania wanaosoma Diploma za Kilimo, ukiwapa ujuzi wa vitendo na fursa za masoko.

Baadhi ya wahitimu tayari wameanzisha mashamba yao wenyewe na sasa wanauza malighafi zao moja kwa moja kwa SBL, kuunda mfumo unaounganisha elimu, uzalishaji na fursa za soko.
Zaidi ya kilimo, SBL imetoa fursa za ajira rasmi kwa zaidi ya wananchi 800 wa Kitanzania na ajira zisizo rasmi 140,000 wakinufaika kupitia minyororo yake ya thamani nchini kote.
Wakati wa kikao hicho, Mkurugenzi Mtendaji wa SBL, Obinna Anyalebechi, alisema:
“Kazi yetu haishii tu kwenye utengenezaji wa bia. Kupitia mpango wa Shamba ni Mali na Kilimo Viwanda, tunaimarisha kilimo cha ndani, kuwawezesha wakulima na vijana, na kuunda minyororo thabiti ya usambazaji inayojikita katika jamii za Kitanzania. Kwa kuwekeza kwenye uuzaji wa ndani na maendeleo ya wakulima, tunachangia kwenye kilimo endelevu kinachosaidia viwanda na ukuaji wa uchumi wa taifa.”
Waziri wa Kilimo, Daniel Chongolo, alithamini mchango wa kampuni hiyo, akisema:
“Serikali inakaribisha wadau wakubwa wa sekta binafsi kama Kampuni ya Bia ya Serengeti wanaowekeza moja kwa moja kwa wakulima na vijana wa Kitanzania. Miradi inayochangia uuzaji wa ndani, maendeleo ya ujuzi, na kilimo endelevu ni muhimu kwa kuendeleza ajenda yetu ya kilimo ya kitaifa. Ushirikiano kati ya serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kufanikisha maendeleo ya sekta ya kilimo nchini.”
