Global Publishers
March 17, 2026
0 Comments
Rais wa Marekani Donald Trump usiku wa kuamkia leo Machi 17, 2026 amesema operesheni za kijeshi dhidi ya Iran zimefanikiwa kwa kiwango kikubwa, akidai kuwa uwezo wa kijeshi wa taifa hilo “umeangamizwa kabisa” kufuatia mashambulizi ya pamoja ya Marekani na Israel.
Trump alitoa kauli hizo wakati akizungumza mwanzoni mwa hafla moja rasmi, ambapo pia alisisitiza kuwa mashambulizi hayo yamesababisha kupungua kwa kiasi kikubwa kwa mashambulizi ya ndege zisizo na rubani (drones) ambazo Iran imekuwa ikizirusha kuelekea mataifa jirani.
Kwa mujibu wa Trump, vikosi vya Marekani vinaendelea kulenga vituo vya uzalishaji wa silaha pamoja na malengo ya kijeshi ya majini ya Iran, hatua ambayo amesema imepunguza uwezo wa kijeshi wa taifa hilo.
Katika hotuba yake, Trump pia alirudia wito kwa washirika wa Marekani kuungana kusaidia kulinda na kufungua njia ya bahari ya Strait of Hormuz, ambayo ni mojawapo ya njia muhimu zaidi duniani kwa usafirishaji wa mafuta.
Njia hiyo ya bahari hupitisha takribani sehemu kubwa ya mafuta ya dunia, hivyo usalama wake una athari kubwa kwa uchumi wa dunia pamoja na siasa za ndani za Marekani.
Trump alionya kuwa Marekani itakumbuka ni nchi gani zilisimama upande wake katika mzozo huo, akisisitiza umuhimu wa ushirikiano wa kimataifa katika kulinda usafirishaji wa mafuta kupitia njia hiyo.
Hata hivyo, hotuba ya Trump haikutoa taarifa nyingi mpya, kwani sehemu kubwa ya kauli hizo tayari alizieleza alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari alipokuwa akirejea kutoka Florida usiku uliopita.