Serikali imedhamiria kuwa Kampasi ya Mloganzila ya Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) itakuwa mji wa kitaaluma na tiba, ikijumuisha vituo vya umahiri vitakavyotoa huduma za matibabu, elimu na utafiti ili kuimarisha sekta ya afya na elimu ya juu nchini.
Hatua hiyo, inatokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea katika Kampasi hiyo, pamoja na uwepo wa kituo cha umahiri cha magonjwa ya moyo na mishipa ya damu ambacho ni cha Kipekee Afrika Mashariki.
Ameongeza kuwa Serikali imetenga dola za Marekani milioni 83 kwa ajili ya kujenga hospitali ya tiba ya magonjwa hayo ikiwa ni sehemu ya Kituo hicho ili kuwezesha kufanya utafiti kutoa mafunzo kwa vitendo na pia huduma kwa wagonjwa.
Aidha, Serikali imekamilisha mkakati wa kuanzisha kituo cha umahiri cha tiba ya kinywa na meno cha Afrika Mashariki .
Akizungumza Machi 17,2026 jijini Dar es Salaam katika ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof. Adolf Mkenda, ameeleza kuwa, juhudi hizo zinatokana na maono ya Mhe. Rais kuifanya Tanzania kuwa kitovu na taaluma za tiba katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na pia kuhakikisha kama Taifa linazalisha wataalamu na wabobezi wa kutosha kuhudumia watanzania wageni kutoka nje wanaokuja kupata huduma.
‘‘’Lengo ni kufanya Kampasi ya Mloganzila kuwa na vituo vingi vya umahiri katika nyanja mbalimbali za tiba na tofauti ya vituo hivi na hospitali ni kwamba, vitafanya utafiti, mafunzo na kutoa huduma ya tiba, ” Amesema Waziri Mkenda.
Prof. Mkenda ameongeza kuwa, Serikali pia inapanga kuanzisha kituo cha umahiri cha matibabu ya saratani ili kupanua wigo wa huduma za kibingwa nchini.
.jpeg)
.jpeg)

