Na Mwandishi wetu
Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (TASAC) limewataarifu wananchi wanaotumia usafiri kwa njia ya maji kutumia vyombo vya usafiri majini vilivyoidhinishwa kubeba abiria na kuepuka kupanda vyombo vya mizigo ambavyo haviruhusiwi kubeba abiria.
Kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa na TASAC, wananchi wanahimizwa kuchukua tahadhari kufuatia visa vinavyoripotiwa vya baadhi ya wananchi kupanda vyombo vya mizigo kinyume cha sheria, jambo linaloongeza hatari ya ajali na kuathiri usalama wa maisha.
TASAC imeeleza kuwa vyombo vya mizigo havijaundwa wala kuidhinishwa kwa kubeba abiria, hivyo kuvitumia kinyume na masharti kunazidisha hatari, hasa wakati wa hali mbaya ya hewa au safari za usiku.
Taarifa hiyo imehimiza kuwa kila chombo cha usafiri majini kinapaswa kutumika kwa madhumuni yake yaliyoidhinishwa kisheria. Wamiliki na waendeshaji wanatakiwa kuzingatia kanuni za usalama ili kulinda maisha ya abiria na mali zao.
TASAC pia imewataka wananchi kuhakikisha wanapanda vyombo vinavyotambulika rasmi, vilivyo na vifaa vya usalama ikiwemo majaketi okozi, na vinazingatia idadi halali ya abiria. Aidha, TASAC imeonya kuwa hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wamiliki au waendeshaji watakaokiuka sheria kwa kubeba abiria kwenye vyombo vya mizigo au kuvuka idadi halali ya abiria.
TASAC inaendelea kutoa wito kwa wananchi kushirikiana na mamlaka husika katika kuhakikisha usalama wa usafiri majini unazingatiwa kwa kufuata sheria na taratibu zilizowekwa.