Mwanza. Serikali ya Tanzania imesisitiza kuwa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) haujasimama, huku ikiendelea kuunganisha mradi huo na usafiri wa majini kupitia meli ya MV Umoja ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo ndani na nje ya nchi.
Kauli hiyo imetolewa kufuatia mijadala ya wananchi kuhusu kasi ya miradi ya kimkakati, baadhi wakidai imekwama, jambo ambalo Serikali imelikanusha.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Machi 22, 2026 jijini Mwanza, Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa alisema ujenzi wa SGR unaendelea katika vipande mbalimbali kama ilivyopangwa, akibainisha kuwa ni mradi mkubwa wenye thamani ya dola bilioni 12 (takribani Sh31 trilioni).
Alisema lengo ni kukamilisha reli hiyo ifikapo mwaka 2028 na kufikia mikoa yote iliyopangwa ikiwemo Mwanza. Ujenzi unaendelea katika vipande vya Mwanza–Isaka (asilimia 68), Makutupora–Tabora (asilimia 15), Tabora–Isaka (asilimia 8) na Tabora–Kigoma (asilimia 10).
Katika kuimarisha usafiri, Msigwa alisema meli ya MV Umoja, iliyokuwa ikisafirisha mabehewa kati ya Mwanza na Uganda kupitia reli ya zamani (MGR), imekarabatiwa kwa gharama ya Sh22.9 bilioni na sasa iko tayari kwa huduma.
Aliongeza kuwa Serikali inajenga meli mpya mahususi kwa SGR ili kuruhusu mizigo kutoka Dar es Salaam kuingia moja kwa moja kwenye meli na kusafirishwa kwenda masoko kama Port Bell na Kisumu.
Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa kuunganisha mifumo ya usafiri ili kuongeza ufanisi, kupunguza gharama na kuifanya Tanzania kuwa kitovu cha biashara Afrika Mashariki na Kati.
Kuhusu MV New Mwanza, alisema tayari imeanza kutoa huduma Ziwa Victoria, ikiwa na uwezo mkubwa wa kubeba abiria na mizigo. Aliwahimiza wananchi na wawekezaji kutumia fursa za biashara na utalii zitokanazo na uwekezaji huo.
Aidha, Serikali inaendelea kuboresha bandari katika maziwa ya Victoria, Tanganyika na Nyasa ili kuongeza ufanisi wa usafirishaji.
Msigwa alisisitiza kuwa Serikali imeweka miundombinu bora, hivyo ni jukumu la wananchi na sekta binafsi kutumia fursa hizo kukuza biashara na uchumi wa nchi.
