Global Publishers
March 24, 2026
0 Comments
Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Bagher Ghalibaf, amekanusha vikali madai ya kuwepo kwa mazungumzo yoyote kati ya Iran na Marekani, akipinga taarifa zilizosambazwa na vyombo vya habari vya Israel kwamba yeye ndiye anayehusika katika mazungumzo hayo ya siri na wajumbe wa Rais wa Marekani Donald Trump.
Akizungumza kwa msimamo mkali, Ghalibaf alisema wazi kuwa hakuna mazungumzo yoyote yaliyofanyika kati ya Tehran na Washington, akisisitiza kuwa taarifa hizo ni za uongo na zinalenga kupotosha hali halisi ya mambo.
Kauli yake imekuja wakati hali ya kisiasa na kijeshi katika eneo la Mashariki ya Kati ikiendelea kuwa tete kufuatia mvutano unaoendelea kati ya Iran, Marekani na Israel.
Ghalibaf alisisitiza kuwa wananchi wa Iran wanataka kile alichokiita “adhabu kamili na ya fedheha” dhidi ya wale aliowataja kama wachokozi, akimaanisha wazi Marekani na Israel.

Kauli hiyo inaonyesha msimamo mkali wa uongozi wa Iran katika kukabiliana na mashinikizo ya nje pamoja na vitisho vya kijeshi vinavyoendelea kuripotiwa katika eneo hilo.
Aidha, aliongeza kuwa viongozi wote wa Iran wanasimama kwa mshikamano mkubwa wakimuunga mkono kiongozi wao pamoja na wananchi hadi pale malengo yao yatakapofikiwa.
Katika kauli hiyo, alionekana kumrejea kiongozi mkuu mpya wa Iran, Mojtaba Khamenei, akisisitiza kuwa hakuna mgawanyiko ndani ya uongozi wa nchi hiyo licha ya shinikizo la kimataifa.
🔴 Tufuatilie kupitia YouTube ya Global TV, like, comment ili kuendelea kuhabarika kila siku kwa habari mbalimbali zenye ukweli na uhakika.