Mwenyekiti kitongoji auawa K’njaro, mtuhumiwa akimbia na kichwa chake

Moshi. Polisi Mkoa wa Kilimanjaro linamshikilia mkazi wa Kijiji cha Masaera, Reginald Riwa kwa madai ya kumuua kwa kumtenganisha kichwa na kiwiliwili, Mwenyekiti wa kitongoji cha Masaera, Ezekiel Temu (62) huku akikimbia na kichwa chake.

Kamanda wa Polisi mkoani humo (RPC), Simon Maigwa amethibitisha kutokea kwa tukio hilo ambalo amesema limetokea leo Jumanne, Machi 24, 2026 huku akidai chanzo ni kutokana na tatizo la afya ya akili kwa mtuhumiwa huyo.

“Leo Machi 24 huko Kitongoji cha Masaera, Ezekiel Temu, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Masaera ameuawa kwa kukatwa na kitu chenye ncha kali kwa kutenganishwa kichwa na kiwiliwili,” amedai Kamanda Maigwa.

Kamanda Maigwa amedai mtuhumiwa alimkimbiza marehemu na kisha kumkata shingo na kisha kuondoka na kichwa cha marehemu.

“Mtuhumiwa alimkimbiza marehemu na alipomkamata alimkata na kitu chenye ncha kali, na kutenganisha kichwa na kiwiliwili na kisha kukimbia na kichwa cha marehemu huku akikining’iniza baada ya kufunga na mkanda wa suruali aliyokuwa amevaa marehemu,” amedai.

Aidha, Kamanda Maigwa amesema mtuhumiwa amekamatwa kwa hatua zaidi za kisheria.

Kamanda Maigwa, amesema mwili wa marehemu umehifadhiwa Hospitali ya Kilema ukisubiri uchunguzi wa daktari na taratibu nyingine.