Dar es Salaam. Zaidi ya wanafunzi 62,000 nchini wamenufaika na matumizi ya nishati safi ya kupikia kutokana na usakinishaji wa majiko ya kisasa katika shule na taasisi za umma zaidi ya 45, huku idadi ya majiko ikizidi 170.
Hatua hiyo imechukuliwa kupitia programu ya CookFund, inayofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU) na kutekelezwa kwa ushirikiano kati ya Serikali ya Tanzania na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Mitaji (UNCDF).
Hayo yamesemwa leo Alhamisi, Machi 26, 2026, katika hafla ya makabidhiano ya msaada huo iliyofanyika katika Shule ya Msingi Bunge, jijini Dar es Salaam, ikionesha hatua muhimu katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, pamoja na kukabiliana na changamoto ya ukataji miti.
Akizungumza katika hafla hiyo, Naibu Waziri wa Nishati, Salome Makamba, amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia ni kipaumbele cha kimkakati cha Taifa katika kulinda mazingira, kuboresha afya ya jamii, na kuongeza ufanisi wa kiuchumi.
Amesema kwa kuzipatia shule na taasisi za umma teknolojia za kisasa za kupikia, Serikali inalenga kupunguza hewa chafuzi, kulinda rasilimali za misitu, na kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi.
“Serikali itaendelea kushirikiana na wadau wa maendeleo ili kupanua upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa kuzingatia Mkakati wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia wa mwaka 2024 hadi 2034,” amesema Naibu Waziri Makamba.
Jitihada za kuhamasisha matumizi ya nishati safi nchini zinaongozwa na Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za Serikali, zikiwemo Ofisi ya Waziri Mkuu – Tamisemi, Wizara ya Maliasili na Utalii, na Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira.
Mpango huo unalenga taasisi zinazohudumia watu zaidi ya 100 kwa wakati mmoja, hususan shule, ili kuondokana na matumizi ya nishati zisizo rafiki kwa mazingira, kama kuni na mkaa.
Akizungumza kwa niaba ya Umoja wa Ulaya, Mkuu wa Ushirikiano nchini Tanzania, Marc Stalmans, amesema mpango huo ni sehemu ya juhudi za kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kusaidia mpito kuelekea matumizi ya nishati safi.
“Tunasaidia watu kuhamia kwenye mbinu endelevu zinazolinda mazingira huku zikichochea ukuaji wa uchumi, kuongeza ajira, na kuboresha upatikanaji wa nishati katika sekta mbalimbali,” amesema.
Kwa upande wake, Mshauri Mkuu wa Masuala ya Kiufundi wa UNCDF, Peter Malika, amesema programu hiyo imewekeza Dola milioni 10.1 za Marekani katika biashara ndogo na za kati 102, pamoja na kusaidia taasisi 45 katika wilaya 14 za mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma, na Mwanza.
Amesema matumizi ya nishati safi ya kupikia yana mchango mkubwa katika kupunguza utegemezi wa kuni na mkaa, huku yakiboresha usalama, afya, na ufanisi katika shughuli za upishi shuleni.
Kwa mujibu wa wataalamu, matumizi ya kuni na mkaa huchangia uzalishaji wa chembechembe hatarishi zinazosababisha magonjwa ya mfumo wa upumuaji, ikiwemo pumu na saratani ya mapafu.
Kupitia CookFund, teknolojia mbalimbali za nishati safi zimeanza kutumika, zikiwemo majiko ya umeme, majiko ya bayoethanoli, majiko banifu, pamoja na matumizi ya gesi na mkaa mbadala.
