******
Benki ya I&M imeendelea kupanua uwekezaji wake katika sekta ya fedha baada ya kufungua rasmi tawi lake la tisa katika eneo la Palm Village, Mikocheni jijini Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kusogeza huduma za kifedha karibu na wananchi na kuchochea ujumuishaji wa kifedha kwa wateja wa rejareja na wafanyabiashara wadogo na wa kati.
Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Afisa Mtendaji Mkuu na Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Zahid Mustafa, amesema hatua hiyo inaonesha dhamira ya benki kuendelea kuwekeza nchini na kusaidia ukuaji wa uchumi ,amesema Tanzania ni soko muhimu kwa benki hiyo na kwamba wataendelea kupanua huduma na kuleta suluhisho bunifu za kifedha zinazokidhi mahitaji ya wateja.
Kwa upande wake, Mkuu wa Huduma za Rejareja na Kidijitali, Simon Gachahi, amesema benki inapanga kuongeza idadi ya matawi hadi kufikia 18 ndani ya miaka mitatu ijayo ili kuongeza upatikanaji wa huduma za benki, huku ikiendelea kutoa bidhaa nafuu ikiwemo miamala ya bure kutoka benki kwenda simu na mikopo ya ununuzi wa mali yenye riba ya asilimia 9 kwa ajili ya kukuza biashara.
Aidha, benki hiyo imeendelea kuwekeza katika huduma za kidigitali ikiwemo benki kupitia WhatsApp na ushirikiano wake na Airtel kupitia huduma ya “Kamilisha”, hatua inayowezesha upatikanaji wa mikopo kwa mamilioni ya Watanzania na kuchochea ukuaji wa uchumi jumuishi hasa kwa wanawake na vijana.









