Taifa Stars imecheza mchezo wake wa kwanza wa Michuano ya Fifa Series na imepoteza kwa bao 1-0 dhidi ya nchi ndogo kisoka Liechtenstein.
Mchezo huu ulioanza taratibu huku Stars ikipoteza nafasi nyingi za wazi kipindi cha kwanza ulifanya kwenye Uwanja wa Pele nchini Rwanda na kuhudhuriwa na mashabiki wa wastani.
Hii ni mara ya pili Stars inashiriki michuano hiyo ambayo imekuwa ikisimamiwa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), mara ya kwanza timu hiyo ilipoteza mchezo mmoja dhidi ya Bulgaria kwa bao 1-0 na kushinda dhidi ya Mongolia kwa mabao 3-0.
Katika mchezo wa jana, Stars ilianza kwa kasi huku kiungo Feisal Salim ‘Fei Toto’ akitawala kipindi cha kwanza kwa kutengeneza nafasi kadhaa kwa Selemani Mwalimu na Kelvin John lakini wote wawili walishindwa kuweka mpira kimiani.
Kipindi cha pili kocha wa Stars Miguel Gamondi, alifanya mabadiliko kadhaa kwenye timu yake ambayo ilionyesha utulivu wa hali ya juu kwenye eneo la kiungo, lakini kosa moja ambalo mabeki wa Stars walifanya lilimfanya mshambuliaji wa Liechtenstein Hasler Saglam, kuifungia nchi yake bao katika dakika ya 55 baada ya kuambaa na mpira huku mabeki wa Stars wakifikiri ameotea na kufunga kwa ustadi wa hali ya juu.
Liechtenstein ambayo ipo nafasi ya 198 kwa ubora wa viwango vya Fifa pia ni nchi ndogo ikiwa na wastani wa wananchi 40,128, imefanikiwa kufunga bao baada ya kucheza michezo miwili bila kuliona lango la mpinzani wake.
Huu ulikuwa mchezo wa kwanza wa Gamondi tangu alipopewa mkataba wa miaka miwili wa kuiongoza timu hiyo ambayo itashiriki michuano ya AFCON 2027, ambayo inaandaliwa kwa ushirikiano wa Tanzania, Kenya na Uganda.
Sasa Stars ambayo inashika nafasi ya 110 kwenye viwango cha FIFA itacheza dhidi ya Macau ambayo kwenye mchezo wa awali ilipoteza kwa mabao 4-1 dhidi ya Aruba, wakati Liechtenstein ikivaana na Aruba.