Kipanga yazitaka alama tatu za Zimamoto FC

UTAMU wa Ligi Kuu Zanzibar unarudi kesho Jumamosi Machi 28, 2026, ambapo Mafunzo itatoana jasho na KVZ huku Kipanga ikivaana na Zimamoto, keshokutwa Jumapili Machi 29, 2026.

Akizungumza na Mwanaspoti, Kocha Mkuu wa Kipanga, Khamis Hassan Makame, amesema wamejiandaa kuhakikisha wanaibuka na ushindi dhidi ya Zimamoto baada ya kushuhudiwa mzunguko wa kwanza zikitoka suluhu.

Kocha huyo, amesema hadi kufikia sasa, mazoezi ya ndani ya uwanja yameshakamilika kwa asilimia kubwa kwa sababu wameanza kujiandaa mapema kuelekea mechi hiyo.

“Tunafahamu mchezo utakuwa mgumu kwa sababu kila timu ina uhitaji wa alama ili kuzidi kujiweka katika mazingira mazuri,” amesema.

Amesema, walipokutana katika mzunguko wa kwanza, vijana wake walistahili kushinda kwa sababu walitengeneza nafasi nyingi lakini wakashindwa kuzitumia, hivyo hawapo tayari kurudia makosa hayo.

Kocha huyo aliongeza kuwa anakiweka vizuri kikosi ili kupata matokeo mazuri kwani uhitaji wao mkubwa ni ushindi na si kingine.

Amesema wanaiheshimu Zimamoto na wataingia kwa tahadhari ili kufanya vizuri katika mtanange huo.

Zimamoto ipo nafasi ya pili katika msimamo wa Ligi Kuu Zanzibar ikiwa na alama 38 sawa na vinara wa ligi, Fufuni, lakini zinatofautiana mabao ya kufunga na kufungwa, huku Kipanga ikikamata nafasi ya sita.