BoT yaeleza mchango wa mifumo ya malipo katika uchumi

Dar es Salaam. Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) anayeshughulikia Sera za Uchumi na Fedha, Dk Yamungu Kayandabila, amesema kuwa mifumo ya malipo ya Taifa ina mchango mkubwa katika kukuza uchumi jumuishi na kuimarisha ujumuishwaji wa kifedha nchini.

Akizungumza wakati wa ukaribisho kwa wanafunzi wa Shahada ya Uzamili ya Biashara (MBA) kutoka Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, waliotembelea BoT jijini Dar es Salaam, Dk Kayandabila ameeleza kuwa mifumo ya malipo inachangia ukuaji wa uchumi shirikishi kwa kuwezesha malipo, lakini pia ni nguzo muhimu ya uthabiti wa sekta ya fedha.

Amebainisha kuwa mifumo ya malipo yenye ufanisi, iliyo salama na shirikishi huchochea ufanisi wa sera ya fedha kwa kuwezesha uenezaji mzuri wa mabadiliko ya viwango vya riba vya Benki Kuu na kuimarisha udhibiti wa ukwasi ndani ya uchumi.

Dk Kayandabila amesema Benki Kuu imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kisera na kuwekeza katika miundombinu ili kuimarisha na kuboresha mifumo ya malipo, sambamba na kuchochea ubunifu, hususan katika huduma za kifedha za kidijitali na ujumuishwaji wa kifedha.

Akifafanua kuhusu historia ya maboresho hayo, alisema kuwa mchakato wa kisasa wa mifumo ya malipo ulianza katikati ya miaka ya 1990 kama sehemu ya mageuzi mapana ya sekta ya fedha yaliyolenga kuongeza ufanisi, usalama na uthabiti wa mfumo wa fedha.

Aliongeza kuwa mageuzi hayo yaliwezesha kuingia kwa benki binafsi za ndani na za kimataifa, ubinafsishaji wa baadhi ya benki za serikali pamoja na kuondolewa kwa baadhi ya vikwazo katika huduma na bidhaa za kifedha.

Kwa mujibu wa Dk. Kayandabila, mwaka 1996 BoT ilianzisha mradi wa Maboresho ya Mifumo ya Malipo ya Taifa uliolenga kubadilisha mfumo wa zamani uliotegemea zaidi fedha taslimu na karatasi kuwa mfumo wa kielektroniki unaoendana na viwango vya kimataifa.

Amekumbusha kuwa kabla ya maboresho hayo, matumizi ya fedha taslimu yalitawala, huku hundi zikichukua hadi siku 14 kukamilisha miamala mikoani na siku 7 jijini Dar es Salaam, hali iliyokuwa ikichelewesha shughuli za kiuchumi.

Aidha, amesisitiza kuwa BoT inaendelea kufuatilia maendeleo ya teknolojia za mifumo ya malipo duniani na kushirikiana na wadau wa kikanda na kimataifa ili kunufaika na ubunifu huo, huku ikiendelea kulinda uthabiti wa sekta ya fedha, uadilifu wa mifumo na maslahi ya watumiaji.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Mifumo ya Malipo ya Taifa, Lucy Shaidi, akielezea hatua muhimu zilizofikiwa katika safari ya kuendeleza mifumo ya malipo hadi kufikia mwaka 2025, anasema kuwa kumekuwapo na ukuaji wa kasi wa malipo ya papo kwa papo, huduma za fedha kupitia simu za mkononi, pamoja na mifumo ya malipo inayoweza kuunganishwa.

Amebainisha kuwa maendeleo hayo yanaendelea kuichochea Tanzania kuelekea katika mfumo wa fedha uliojumuishi zaidi, wenye ufanisi na unaotegemea kwa kiasi kikubwa teknolojia za kidijitali.

Miongoni mwa mafanikio yaliyotajwa katika mifumo ya malipo ni kuanzishwa kwa Mfumo wa Malipo ya Papo kwa Hapo (Tanzania Instant Payment System – TIPS), unaoruhusu watumiaji wa huduma za fedha kutuma na kupokea fedha papo hapo, bila kujali taasisi ya kifedha wanayotumia.